WANANCHI WATAKIWA KUACHA TABIA YA KUHARIBU MIUNDOMBINU YA MAJI BADALA YAKE KUILINDA🇹🇿 - MAIPAC MEDIA TANZANIA

Breaking

MAIPAC MEDIA TANZANIA

A Centre for Indigenous and Pastoralists Community Informations




Wednesday 2 October 2024

WANANCHI WATAKIWA KUACHA TABIA YA KUHARIBU MIUNDOMBINU YA MAJI BADALA YAKE KUILINDA🇹🇿

 





Na Elinipa Lupembe, ARUSHA 


maipacarusha20@gmail.com


Wananchi Mkoani Arusha, wametakiwa kuacha tabia ya kuharibu miundombinu ya maji inayopita kwenye maeneo yao  badala yake kuitunza na kuilinda ili kuwa na uhakika wa huduma ya maji wakati wote.


Rai hiyo imetolewa na Meneja wa Wakala wa Maji na Usafi wa Wa Mazingira Vijijini Mkoa wa Arusha, Mhandisi  Joseph Emmanuel Makaidi, kufuatia uharibifu mkubwa wa miundombinu ya maji uliofanywa na baadhi ya wafugaji kwa kukatwa kwa bomba kuu linalopeleka maji kwenye Skimu ya MONALO inayohudumia vijiji vya kata ya Moita Bwawani wilaya ya Monduli na kusababisha Kijiji cha Moita Bwawani kukosa maji  kwa takribani wiki mbili sasa na kuzua taharuki kwa jamii.


Amewataka wakazi wa Arusha kuwa na utamaduni wa kutunza miundombinu ya Maji ili kuhakikisha upatikanaji wa kutosha wa maji safi na salama na kutoiingiza Serikali kwenye gharama kubwa za matengenezo ya miundombinu ilinayoharibiwa.


Serikali inatumia fedha nyingi kutekeleza Miradi ya maji, tutambue miradi hiyo inatengenezwa kwa gharama kubwa sana, inapoharibiwa kwa makusudi tunaisababishia Serikali hasara ya kurudia kutengeneza ili hali fedha hizo zingefanya kazi nyingine, lakini zaidi husababisha adha kubwa ya kukosekana kwa huduma ya maji" Amefafanua Mhandisi huyo.


Aidha, amezitaka Serikali za Vijiji  kuwa na mpango wa ulinzi shirikishi kwenye maeneo yao ili kusaidia katika ulinzi wa miundombinu hiyo ya maji pamoja na kuvisimamia vyombo vya watumia maji kuweka utaratibu mzuri wa kulipia huduma za maji ili Skimu za maji ziweze kujiendesha na kuwa endelevu.


Ikumbukwe kuwa, Septemba 27, 202 wanawake wa  Kijiji cha Moita Bwawani, waliandamana kuelekea kwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha kulalamikia ukosefu wa maji katika kijiji chao, ukosefu uliosababishwa  baadhi ya wananchi kukata bomba kuu .


Hata hivyo, RUWASA inafanya jitihada za kurejesha huduma hiyo ya Maji kwenye Kijiji cha Moita huku jitihada mbalimbali zinafanyika ngazi ya Mkoa ili kutimiza maagizo ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe.  Paul Christian Makonda, aliyeagiza RUWASA kutenga miundombinu kwaajili ya upatikanaji ya mifugo kwenye maeneo ya wafugaji.


Mwisho

No comments: