LHRC WAITAKA SERIKALI KUUNDA TUME MAALUM KUHAKIKI MIPAKA YA HIFADHI NA WANANCHI ILI KUPUNGUZA MIGOGORO. - MAIPAC MEDIA TANZANIA

Breaking

MAIPAC MEDIA TANZANIA

A Centre for Indigenous and Pastoralists Community Informations




Friday 8 September 2023

LHRC WAITAKA SERIKALI KUUNDA TUME MAALUM KUHAKIKI MIPAKA YA HIFADHI NA WANANCHI ILI KUPUNGUZA MIGOGORO.


Dkt. Anna Henga Mkurugenzi mtendaji wa LHRC akizungumza na waandishi wa habari jijini Arusha mapema leo


Na: Andrea Ngobole, Arusha

 

maipacarusha20@gmail.com

 

Kituo cha sheria na haki za binadamu (LHRC) kimeitaka serikali kuunda tume maalaum au kikosi kazi kitakachofanya kazi ya uhakiki wa mipaka katika maeneo yote ya hifadhi ambayo yamekuwa yakisababisha migogoro kati ya wananchi na mamlaka za hifadhi.

 

Mkurugenzi mtendaji wa kituo cha sheria na haki za Binadamu nchini, Dkt Anna Henga amesema hayo jijini Arusha leo alipokuwa akisoma taarifa ya hali inayoendelea Ngorongoro ya ukiukwaji wa haki za binadamu wakati wa utekelezaji wa uhamishaji wa wakazi wa ngorongoro kweda Msomera.


Amesema wao kama watetezi wa haki za binadamu hawapingi kuhamishwa kwa wakazi walioridhia kuhama isipokuwa zoezi la uhamishaji wakazi hao lisitumike kuwanyanyasa wakazi ambao hawajaridhia kuhama.


Amesema ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu unaonekana Zaidi katika huduma za elimu na afya ambapo watoto 24,000 hawajapata huduma yoyote ya chanjo kama watoto wengine nchini, wanawake wajawazito 5,700 hawajapata huduma, matibabu, chanjo na ushauri wa afya wakati wa ujauzito, wagonjwa 145 wenye TB sugu hawajapata dawa na wagonjwa 84 wenye VVU hawajaweza kupata dawa za kufubaza virusi vya ukimwi na hivyo kutishia uhai wao.


Amesema adha hiyo imetokana na serikali kusitisha huduma za kijamii kwa kutoendeleza miradi na kusitisha huduma kwa kuondoa fedha katika taasisi mbalimbali na kutopanga bajeti ya fedha 2022/23 na 2023/24 kama kuondolewa kwa fedha za vifaa tiba milioni 500 za zahanati ya Nainokanoka kupelekwa Msomera, million 80 za ujenzi wa kitengo cha wagonjwa wa nje zahanati ya Osinoni kuondolewa na fedha za zahanati nyingine zimeondolewa tangu mwezi April 2022.


Ameendelea kusema kuwa serikali imeondoa shilingi milioni 500 kwa hospitali ya Endulen kama ruzuku toka mwaka 2020, na kuathiri wananchi 100,000 wa tarafa ya Ngorongoro wanaoitegemea hospitali hiyo.


Ukiukwaji mwingine wa haki za binadamu ulioanishwa katika taarifa hiyo ni huduma za Elimu ambapo Jumla ya shilingi million 256 za shule za msingi za Irkipori, Endulen na Ereko na kuhamishiwa shule misngi Msomera,  milioni 790 za ujenzi wa bweni, shule mpya ya Endulen na madarasa mapya nazo zimeondolewa.


Taarifa hiyo Imesema kuwa jumla ya shilingi milioni 720 za ujenzi wa madarasa, mabweni na mabwalo katika shule za sekondari za Ngorongoro Girls, Embarway na Nainokanoka zimeondolewa na kusitisha mpango wa ujenzi katika shule hizo.


Huduma za ujenzi wa miradi ya maji katika kata za Ngoile million 200, kata ya Masamburai million 151, kata ya Olbalbal milioni 200 na kata ya Alaililai million 146 zimeondolewa na kusababisha adha kwa wananchi waliopo katika kata hizo.


Amesema kuwa kwa takribani mwezi sasa wananchi 48 wamekamatwa, kushikiliwa Zaidi ya muda unaoruhusiwa kisheria bila kupewa haki ya kuwasiliana na familia wala wanasheria wao, viongozi wa ngazi zote kata ya Endulen wamekamatwa kwa madai ya kuhasisha wananchi wao kudai huduma za kijamii.


Amesema kituo hicho kinatoa wito kwa serikali kuwa mchakato unaoendelea wa kuhamisha wananchi usitumike kuwanyanyasa, kuwanyima huduma za kibinadamu, kuwashurutisha kuondoka pasi na ridhaa yao.


Kuzingatia haki za binadamu wakati wa utekelezaji wa amri za kuwaondoa na kuwahamisha wananchi katika hifadhi, serikali isimamie ahadi yake kuwa wananchi wanaohamishwa Ngorongoro ni wale waliokubali wenyewe kuhama na wale wasiotaka kuhama waachwe na wapewe huduma za kibinadamu kama watanzania wengine.


Amesisitiza kuwa tume ya haki jinai hasa jeshi la Polisi na majeshi usu iweze kufanyiwa kazi mapema ili kuimarisha ulinzi wa haki za binadamu.

 


 

 

 

 

No comments: