Afungwa miaka 23 Jela kutokana na kujihusisha na ujangili waTwiga na kufanya biashara ya nyama za Twiga - MAIPAC MEDIA TANZANIA

Breaking

MAIPAC MEDIA TANZANIA

A Centre for Indigenous and Pastoralists Community Informations




Thursday 9 November 2023

Afungwa miaka 23 Jela kutokana na kujihusisha na ujangili waTwiga na kufanya biashara ya nyama za Twiga





Mwandishi wetu, Babati


 

maipacarusha20@gmail.com


Mahakama ya Hakimu Mkazi mfawidhi wa wilaya ya Babati mkoa Manyara, imemuhukumu kwenda jela miaka 23  , Amos Benard  Mtinange maarufu kwa jina la Meja baada ya kutiwa hatiani kwa makosa mawili ujangili wa Twiga na kuuza nyama za Twiga kinyume cha sheria


Meja alikamatwa  April 21 mwaka 2022,  saa kumi na moja jioni  maeneo ya mfulwang'ombe kwenye Kambi ya samaki Kijiji cha Vilima vitatu, ndani ya eneo la hifadhi ya jamii ya wanyamapori ya Burunge wilayani Babati, mkoa wa Manyara baada ya kusakwa muda mrefu kutokana na kujihusisha na ujangili wa Twiga na kufanya biashara ya nyama za Twiga.


Alikamatwa kutokana na mtego  ulioandaliwa na askari wa Mamlaka ya Usimamizi Wanyamapori (TAWA), Jeshi la polisi, Askari wa Burunge WMA na askari wa Taasisi ya Chem chem association ambayo imewekeza shughuli za Utalii katika eneo hilo.


Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa mahakama ya wilaya ya Babati, mkoa wa Manyara, Victor Kimario alisema,  mahakama imemtia hatiani  Meja baada ya kujiridhisha pasi na shaka kuwa amekuwa akijihusisha na ujangili wa Twiga na kuuza nyama za Twiga.


Alisema ili kukomesha matukio ya ujangili nchini, Mahakama inamuhukumu kutumikia kifungo cha miaka 23 jela.


Kabla ya hukumu hiyo, Meja aliomba mahakama kumpunguzia adhabu kwani anafamilia ambayo inamtegemea.


Hata hivyo, Waendesha Mashitaka wa Serikali   Benedict Mapunda,na Mawakili wa Mamlaka ya Usimamizi Wanyamapori(TAWA) Getrude Kariongi na  Shahidu Kajwagya,walipinga kupunguziwa adhabu mtuhumiwa huyo.


Wakili Kariongi alisema kesi  inayomkabili mtuhumiwa huyo ni ya uhujumu uchumi na ambacho amekuwa akifanya muda mrefu ni kuuwa Twiga ambao ni kivutio cha Utalii nchini lakini pia mnyama huyo anachangia pato la taifa.


Alisema wanyamapori huchangia kupatikana fedha za kigeni ambazo ndizo zinachangia  kupatikana fedha za miradi ya serikali ikiwepo ujenzi wa shule, kuchangia gharama za afya na nyingine.

Katika kesi hiyo, Jamuhuri ilikuwa na mashahidi saba  ambao walikuwa ni mtunza vielelezo vya polisi, Askari wawili walioshiriki kumkamata , Mtambuzi na mtathimini wa nyara za serikali, Mtaalamu kutoka Forensic, Mpelelezi wa kesina Mlinzi wa Amani ambaye alikuwa ni hakimu.


 *Wapongeza hukumu* .


Baadhi ya wadau wa sekta ya Utalii na Uhifadhi, wilayani Babati, wakizungumza na waandishi wa habari baada ya hukumu hiyo, walipongeza mahakama kwa uamuzi huo.


Lazaro Peter ambaye ni mhifadhi, alisema biashara ya nyama za Twiga ilikuwa imeshamiri wilayani Babati, kutokana na uwindaji haramu na sasa wanaimani itakuwa imekomeshwa.


“Unajua Twiga wapo wengi sana eneo la Burunge WMA sasa majangili imekuwa ni rahisi kuwawinda na kufanya biashara ya Nyama sasa Meja alikuwa mmoja wa watuhumiwa wakubwa na anatuhumiwa kuuwa zaidi ya Twiga watano kila mwezi”alisema


Meneja wa taasisi ya  Chem chem  association, ambaye imewekeza katika eneo hilo, Clever Zulu alisema kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo na kutiwa hatiani ni  jitihada ambazo zimefanywa na askari wa Wanyamapori.


Zulu amesema kabla kufanikiwa kukamatwa majangili katika eneo hilo,  askari hao wa Wanyamapori walipata mafunzo maalum kutoka kwa maafisa wa TAWA na jeshi la polisi  jinsi ya kufanya upelelezi, upekuzi na ukamataji wa majangili.


"Haya ni mafanikio makubwa kwetu katika kulinda rasilimali tunawapongeza askari kwa kuonesha ufanisi baada ya mafunzo"amesema


Zulu amesema Chem chem association ambayo inatumia zaidi ya sh 400 milioni kila mwaka katika kupambana na ujangili katika eneo la Burunge WMA itaendelea kutoa fedha za kupambana na ujangili.



Hadi sasa zaidi ya watuhumiwa 10 wa ujangili wamekamatwa katika eneo hilo na tayari watatu wamehukumiwa vifungo mbali mbali ikiwepo Meja aliyefungwa miaka 23.


No comments: