Na: Mwandishi Wetu, Monduli
maipacarusha20@gmail.com
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Samia Suluhu Hassan amewatunuku Kamisheni maafisa wanafunzi 575 wa Jeshi la wananchi wa Tanzania.
Maafisa hao, kundi la 04/20 wametunukiwa pia Shahada ya Sayansi ya Kijeshi na kundi 70/22 cheo cha Luteni Usu , Katika Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi Monduli ambapo kati yao wanaume ni 482 na Wanawake 93
Maafisa wanafunzi wa Kijeshi 62 wamepata mafunzo chuoni hapo kwa miaka 3 na kuhitimu Shahada ya Sayansi ya kijeshi.
Maafisa wanafunzi 447 wamepata mafunzo ya kawaida ya mwaka mmoja na miongoni mwao maafisa wanafunzi 66 wamepata mafunzo ya urubani kutoka nchi rafiki.
Rais Samia kabla ya kutunuku Kamisheni alikagua gwaride lililoandaliwa na maafisa wanafunzi kutokana na maelekezo ya Mkuu wa chuo cha Mafunzo ya Kijeshi -Monduli Brigedia Jenerali Jackson Mwaseba na kusimamiwa na mkufunzi Mkuu, Kanali Nilinda Duguza.
Mkuu wa Chuo hicho, Brigedia Jenerali Mwaseba alisema, Shahada hiyo ya Sayansi imefanywa kwa mara ya kwanza chuoni hapo pasipo ushirikiano wa kimafunzo na chuo cha Uhasibu Arusha (IAA).
Katika tukio hilo, Rais pia alitoa zawadi kwa maafisa wanafunzi waliofanya vizuri katika mafunzo yao.
Katika kundi la Shahada ya Sayansi ya Kijeshi Mshindi wa Jumla alikuwa ni Mihanzo Rupia Jafari, Mshindi wa Taaluma ,Maria Lyakurwa, Mshindi wa Medani Salia Mkwele ambapo Mshindi wa Jumla wanawake ni Grace Ng'ondya.
Katika kundi la 70/22 waliopewa zawadi kwa kufanya vizuri ni Amour Ubwa Mohamed Afisa mwanafunzi rubani aliyevishwa bawa, Mshindi wa Jumla Dickson Ngenje, Mshindi wa Taaluma Shaban Adam, Mshindi wa Medani Shukuru Saria na mshindi wa Jumla wanawake Nuru Ngabo.
Sherehe hizo zimehudhuriwa pia na Spika wa Bunge Dk Tulia Akson, Mkuu wa Majeshi yaUlinzi, Jenerali Jacob Mkunda, Mnadhimu Mkuu wa JWTZ Luteni Jenerali Salum Haji Othaman, makamanda mbalimbali, majenerali wastaafu, Mawaziri na viongozi mbalimbali wa serikali.
No comments:
Post a Comment