RC MONGELLA AWAASA WANAFUNZI SHULE YA MSINGI MONIC KUSOMA KWA BIDII - MAIPAC MEDIA TANZANIA

Breaking

MAIPAC MEDIA TANZANIA

A Centre for Indigenous and Pastoralists Community Informations




Saturday 11 November 2023

RC MONGELLA AWAASA WANAFUNZI SHULE YA MSINGI MONIC KUSOMA KWA BIDII

 





Na Elinipa Lupembe, Ngorongoro


maipacarusha20@gmail.com



Mkuu wa mkoa wa Arusha amewataka wanafunzi wa shule ya Msingi Monic, Wilaya ya Ngorongoroo,  kutia bidii kwenye masomo yao ili waweze kufaulu na kufikia ndoto zao, kwa kuwa serikali inategemea kupata watalamu wa kulitumikia Taifa hili kupitia wao.


Amesema hayo wakati akizungumza na wanafunzi wa shule hiyo, mara baada ya kukagua mradi wa ujenzi wa vyumba vya madarasa shuleni hapo, mradi uliotekelezwa na Serikali kupitia programu ya BOOST.


Mhe. Mongella amewaasa wanafunzi hao kusoma kwa bidii kwa kuwa serikali yao ya awamu ya sita inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan inawajali kwa kuwawekea mazingira bora na rafiki ya kujifunzia.


Amesema kuwa serikali imejenga madarasa mazuri  ili kila mtoto wa Sale aweze kusoma na kufika ndoto zake za kupata ujuzi na maarifa ya kulitumikia Taifa la Tanzania mara baada ya kuhitimu masomo yake ya shule.


"Serikali inawajengea madarasa mazuri ili msome vizuri, fanyani bidii, bibi yenu mama Samia anataka muwe watalamu wa kulitumikia Taifa lenu, anapostafu kazi ninyi ndio mjekuwa viongozi wa nchi hii, Rais atoke hapa shule ya Monic, msimuangushe".Amesema Mhe. Mongella


Hata hivyo wanafunzi hao wa Monic licha ya kumshukuru Mama Samia wameahidi kusoma kwa bidii na kufia ndoto zao za kuwa watalamu wa kulitumikia Taifa kama yalivyo malengo ya Serikali yao.


Dada Mkuu wa shule, Sinyati Saitabau amemshukuru Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuwajengea madarasa mazuri, yanapendeza ambayo kwa sasa wanasoma vizuri na kuahidi kuhamasisha wenzake kuongeza bidii kwenye masomo ili waweze kufaulu


"Tunamshukuru mama Samia, ametukumbuka wanafunzi wa Monic, madarasa ni mazuri sana yanapendeza na sisi tutasoma sana, kama kiongozi nitawahimiza wenzangu kuongeza bidii kwenye masomo na kufaulu vizuri" Amesema Sinyati.


Naye Mwalimu Mkuu wa shule hiyo amesema kuwa madarasa hayo ni muhimu shuleni hapo kwani yamepunguza msongamano wa wanafunzi darasani na kurahisisha tendo la kujifunza na kufundisha kwa walimu na wanafunzi. 


Aidha amesema kuwa wao kama walimu wameridhishwa na utendaji wa serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia na wanaahidi kufanya kazi kwa weledi ya kuwafundisha wanafunzi ili kufikia malengo ya Serikali na wanafunzi kufikia ndoto zao.

No comments: