Tawiri yaeleza faida ya matumizi ya Teknolojia katika uhifadhi endelevu. Burunge WMA wajipanga pia matumizi ya Teknolojia kuzuia migogoro wanyamapori - MAIPAC MEDIA TANZANIA

Breaking

MAIPAC MEDIA TANZANIA

A Centre for Indigenous and Pastoralists Community Informations




Monday 4 March 2024

Tawiri yaeleza faida ya matumizi ya Teknolojia katika uhifadhi endelevu. Burunge WMA wajipanga pia matumizi ya Teknolojia kuzuia migogoro wanyamapori

 



Mkurugenzi Mkuu TAWIRI, Dk Eblate Ernest Mjingo akifafanua jambo Kwa waandishi wa Habari 


Na: Mwandishi wetu, maipac


maipacarusha20@gmail.com


Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori nchini (TAWIRI) imebainisha kwa vitendo  Matumizi  ya  teknolojia  Katika Uhifadhi  wa Wanyamapori yalivyo na tija katika uhifadhi endelevu.


Akizungumza na waandishi wa habari, Mkurugenzi Mkuu TAWIRI, Dk Eblate  Ernest  Mjingo  amesema teknolojia  mbalimbali  zimerahisisha  tafiti za  wanyamapori nchini kufanyika kwa wakati na kwa usahihi zaidi.


Dk. Mjingo amebainisha miongoni mwa  teknolojia  zinazotumika katika tafiti za wanyamapori  ni pamoja na matumizi ya teknolojia  ya akili mnemba (artificial intelligence)  kuchakata takwimu  na uchambuzi wa picha katika zoezi la kuidadi wanyama (sensa), teknolojia ya  mikanda ya visukuma mawimbi( GPS satellite Collar)  kufuatilia mienendo ya wanyamapori, matumizi ya ndege zisizo na Rubani rubani (Drone) kutatua changamoto ya wanyamapori wakali na waharibifu .


Pia, matumizi  ya helikopta/ndege kuwafuatilia wanyamapori kwa matibabu au kuwarejesha wanyama  maeneo ya hifadhi, kamera za kutega (camera  trap) kubaini  aina ya wanyamapori waliopo katika  maeneo mbalimbali na changamoto za uhifadhi na tekinolojia  ya vinasaba (DNA) kutambua afya ya uzazi wa wanyamapori kwenye mifumo ikolojia mbalimbali. 



Dk.Mjingo amesema awali kabla ya matumizi ya teknolojia  kulikuwa na ugumu katika kufanya  tafiti za wanyamapori baadhi ya maeneo kwani iliwalazimu watafiti kutumia muda mrefu kufanya tafiti, kutumia gharama kubwa, usalama  mdogo .


 " Kwa kutumia teknolojia  ya Akili mnemba (AI) kuchambua  picha na  kuchakata takwimu  imesaidia kutumia nusu ya siku zilizokuwa zinatumika awali sambamba na kupunguza gharama "  ameeleza Dkt. Mjingo


Dk. Mjingo  amebainisha awali  ilikuwa vigumu kufuatlia tabia za wanyamapori kwani wanyamapori wakiona gari au watu mara nyingi hubadili tabia sambamba na ugumu kufuatilia wanyamapori  nyakati za usiku, msimu wa mvua na maeneo yasiyofikika ambapo kwa sasa teknolojia  ya kamera za kutega (camera  trap) inatumika nyakati za mchana na usiku. 


 Ametoa wito kwa wadau   wa uhifadhi  na  utalii ndani  na  nje  ya  nchi  kushirikiana  na  TAWIRI kwa  kuzingatia tafiti za  wanyamapori  ni muhimu  katika  sekta ya uhifadhi  na  utalii  nchini ambapo  pia ametoa  wito kwa mamlaka  za uhifadhi  kutumia  ushauri  wa kisayansi unaotokana na  matokeo  ya tafiti  mbalimbali.


Maadhimisho ya siku ya wanyamapori kitaifa yamefanyika wilayani Babati mkoa Manyara ambapo mgeni Rasmi alikuwa Waziri wa Maliasili na Utalii.


Katika maadhimisho hayo Angellah Kairuki pia ameelezea mikakati ya Wizara yake kuendeleza uhifadhi kwa kujumuisha Teknolojia za kisasa.


Katika utekelezwaji wa Mpango wa matumizi ya Teknolojia za kisasa katika uhifadhi tayari viongozi wa jumuiya ya hifadhi ya Jamii Burunge walipelekwa Ikona WMA kujifunza matumizi ya Technolojia za kisasa kuzuiwa migogoro baina ya Binaadamu na wanyamapori


Katika ziara hiyo ya mafunzo ambayo ilidhaminiwa na Taasisi ya chemchem foundation, viongozi hao wa WMA walipata elimu juu ya matumizi ya nyaya za umeme kuzuiwa wanyamapori wakali na waharibifu kuingia katika makazi ya watu na kufanya uharibifu wa mazao na kusababisha vifo.


Ikona WMA kwa kushirikiana na Taasisi ya Grumet imeweza kupunguza migogoro baina ya wanyamapori na Binaadamu kutokana na kuweka uzio wa umeme kutenga maeneo yaliyohifadhiwa na maeneo ya kijamii 


Ziara ya mafunzo hayo pia ikimshirikisha Mkurugenzi wa Halmashauri ya Babati Anna Mbogo, Maafisa wanyamapori wa mkoa Manyara na Babati ambao wote walijiridhisha umuhimu wa matumizi ya Teknolojia za kisasa katika uhifadhi.


Meneja wa Chemchem, Clever Zulu alisema ziara hiyo imekuwa na manufaa makubwa na wanatarajiwa mafunzo zaidi kutolewa kwa viongozi wa Burunge WMA kuweza kupunguza migogoro baina ya wanyamapori na Binaadamu.

Katibu wa Burunge WMA, Benson Mwaise pia alisema Uongozi wake pia utaandaa ziara nyingine Ikona WMA kujifunza zaidi juu ya utatuzi wa migogoro baina ya wanyamapori na Binaadamu na kuwa na Uhifadhi endelevu 





No comments: