Na Epifania Magingo, Babati
maipacarusha20@gmail.com
Tume huru ya Taifa ya Uchaguzi imewataka watendaji ngazi ya Mkoa wa Manyara kutumia Elimu na ujuzi walioupata kwenye mafunzo ya uandikishaji wa zoezi la uboreshaji wa daftari la kudumu la mpiga kura ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuelekea kwenye Uchaguzi mkuu utakaofanyika mwaka 2025.
Akizungumza katika mafunzo kwa watendaji hao Mjumbe wa tume huru ya Taifa ya Uchaguzi Mheshimiwa Asina A. Omar amesemà watendaji hao wanapaswa kufanya kazi kwa weledi na moyo wa kujituma pamoja na kutumia uzoefu walionao ikiwemo Elimu waliyoipata ili kukamilisha zoezi hilo.
"Matarajio ya tume Kutokana na mafunzo haya kila mmoja wenu atapata elimu na ujuzi wa kutosha utakaowezesha kutekeleza majukumu yake ili kufanikisha uboreshaji wa daftari,mafunzo haya yatahusisha namna ya ujazaji wa fomu pamoja na kutumia mfumo wa kujiandikisha wapika kura".
Aidha,amesema wakati wa uboreshaji wa daftari la kudumu la mpiga kura mawakala na viongozi wa vyama vya siasa hawaruhusiwi kuingilia mchakato wa uboreshaji wa daftari la mpiga kura hapo kituoni.
Naye, Mkaguzi Afisa wa Uhamiaji Mkoa wa Manyara castor Paul Makungu amesema waandikishaji wanapaswa kuwa makini katika zoezi la uandikishaji na kuchukua taarifa muhimu kutoka kwa raia huku wakipaswa kutoa taarifa kwa Jeshi la uhamiaji endapo wakipata wasiwasi wa muadikishwaji.
"Yule muandikishaji akipata changamoto yoyote ile ata akihisi tu huyu sio raia wa Tanzania ni vizuri akawasiliana na Jeshi la uhamiaji ili tuweze kuitatua kwa haraka,tuna ofisi katika ngazi ya Wilaya na Mkoa".
Amesema kwa yeyote ambaye atabainika kudanganya kwa kutoa taarifa zisizosahihi kwa muandikishaji atatuchukuliwa hatua Kali za kisheria.
Zoezi la kujiandikisha katika uboreshaji wa daftari la kudumu la mpiga kura kwa mwaka 2024/2025 linabebwa na kauli mbiu isemayo"KUJIANDIKISHA KUWA MPIGA KURA NI MSINGI WA UCHAGUZI BORA".
No comments:
Post a Comment