SERIKALI YAAHIDI KUSHIRIKIANA NA ASASI ZA KIRAIA KUWALETEA MAENDELEO WANANCHI - MAIPAC MEDIA TANZANIA

Breaking

MAIPAC MEDIA TANZANIA

A Centre for Indigenous and Pastoralists Community Informations




Monday 9 September 2024

SERIKALI YAAHIDI KUSHIRIKIANA NA ASASI ZA KIRAIA KUWALETEA MAENDELEO WANANCHI





Waziri wa Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo akizungumza wakati wa uzinduzi wa wiki ya Asasi za kiraia jijini Arusha Leo 




NA: Mwandishi Wetu, Maipac 

maipacarusha20@gmail.com 


SERIKALI itaendelea kushirikiana na Asasi za Kiraia nchini na kwamba haitakuwa kikwazo kwao katika shughuli zake za kuleta maendeleo, sanjari na kutoa mawazo yatakayojenga zaidi ili kutafuta fursa zilizopo ndani na nje ya nchi.

Hayo yamebainishwa na Waziri wa Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo wakati akifungua Wiki ya Asasi za Kiraia (AZAKI) iliyoanza rasmi leo Septemba 9, 2024 jijini Arusha.

Profesa Mkumbo amesema ni vema sasa Asasi za Kiraia zikashirikiana na serikali katika kutoa maoni yao ikiwemo kukaa meza moja kutatua changamoto zinazoibuka sanjari na kutafuta fursa za masoko ya ndani na nje ya nchi katika kukuza uchumi

Prof. Mkumbo amesema, lengo kuu la serikali ni kuhakikisha ustawi wa watu wote unakuwa, na ili kufika huko ni vema zaidi kujifunza kupitia kwa watu, kuwa wabunifu na kutoa maoni katika kuhakikisha Dira ya Mendeleo ya Taifa ya mwaka 2050 inaleta tija zaidi hususan katika uwekezaji kwenye elimu, miundombinu ikiwemo umeme wa uhakika.


Mkurugenzi Mtendaji wa The Foundation For Civil Society( FCS )Justice Rutenge, akizunguza wakati wa uzinduzi wa Wiki ya AZAKI , jijini Arusha.


‘’AZAKI zihakikishe zinaisemea jamii changamoto ambazo wanaziona na kutatuliwa ili kuisaidia serikali kuzishughulikia na si kuilalamikia kuwa haifanyi kazi ilihali hawajazibainisha ili zifanyiwe kazi na jamii iweze kupata mabadiliko’’. amesema Mkumbo.

Amesema nchi zilizoendelea zimepiga hatua katika maendeleo kwa sababu ya umeme hivyo uwepo wa Bwawa la mwalimu Nyerere nchini Tanzania hadi kukamilika kwake utawezesha umeme kupatikana kwa wingi ikiwemo uchumi kukua kupitia viwanda vinavyozalisha bidhaa ndani ya nchi na kuuza bidhaa hizo nje ya nchi kwa kushirikiana na sekta binafsi hususan za kilimo .

Naye rais wa Foundation For Civil Society (FCS), Dk Stigmata Tenga amesisita kuwa lazima mabadiliko ya watanzania yatokee kupitia AZAKI ambazo ndio husemea wananchi wenye changamoto mbalimbali katika sekta za afya, Elimu, miundombinu ya barabara ikiwemo utoaji wa fursa za fedha kupitia taasisi mbalimbali zinazowawezesha wananchi kujikwamua kimaisha kupitia mikopo yenye riba nafuu na kuongeza kuwa rasilimali watu ni muhimu kuzingatiwa katika kuwaletea wananchi maendeleo.

Wakati huo huo, Mkurugenzi Mkazi wa TradeMark Africa Elibariki Shammy amesema mkakati wa serikali ni kuhakikisha biashara za kidigitali zinakua zaidi kwa kushirikisha vijana kwa kasi kubwa kupitia biashara kwa kuwawekea mazingira rafiki yatakayowasaidia kujikwamua kiuchumi kupitia fursa mbalimbali zilizopo nchini.

Awali Naibu Balozi wa Umoja wa Ulaya (EU), Isabelle Mignucci ameshukuru ushirikiano kati ya serikali ya Tanzania na mashirika mbalimbali unaoleta tija katika maendeleo sanjari na kuhakikisha vijana wanapata fursa za maendeleo kupitia teknolojia na ubunifu unaoleta tija zaidi katika ukuaji wa uchumi.

No comments: