![]() |
Na Epifania Magingo, Manyara
maipacarusha20@gmail.com
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb), akiwa anamuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ameshiriki ibada ya kumsimika Askofu mteule wa Kanisa Anglican Dayosisi ya kiteto, Canon Bethuel Joel Mlula.
Ibada hiyo iliyofanyika leo Machi 9, 2025 katika Kanisa Anglican Dayosisi ya kiteto Wilayani kiteto Mkoani Manyara, na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali akiwemo Mkuu wa Mkoa wa Manyara Queen Cuthbert Sendiga,Job Ndugai ambaye ni Spika mstaafu na Viongozi wa dini.
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amempongeza Askofu Mlula kwa kusimikwa kuwa askofu huku akieleza kwamba Serikali inatambua mchango wa kanisani Anglican katika kushirikiana na Serikali kwenye utoaji wa huduma mbalimbali za kijamii ikiwemo Elimu, Afya na kutoa fursa za maendeleo ya kiuchumi kwa jamii.
Aidha akijibu maombi yaliyowasilishwa na Askofu kuhusu maboresho ya miundombinu ya Barabara wilayani humo, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ameeleza kuwa Serikali imepanga kutekeleza ujenzi wa barabara ya Kongwa-Kibaya-Simanjiro-Arusha kwa kiwango cha lami na tayari Serikali imeshatenga fedha za ujenzi wa kilomita 70 kama sehemu ya utekelezaji wa mradi huo.
Sambamba na hilo Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ameuagiza uongozi wa Mkoa kushughulikia tatizo la uharibifu wa mazingira na migogoro ya wakulima na wafugaji wilayani humo.
Mwisho ametoa wito kwa viongozi wa Dini na Jamii kwa ujumla kusimamia mmomonyoko wa maadili unaoendelea kushamiri kwenye jamii ya Kitanzania
No comments:
Post a Comment