Na Mwandishi wetu, Maipac KIBAHA
maipacarusha20@gmail.com
KAMATI ya kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria imesema katika kipindi hiki uwekezaji umeongezeka kutokana na uhamasiahaji uliofanywa na Rais Samia Suluhu Hassan.
Kamati hiyo imeahidi kutoa ushirikiano wa karibu kuhakikisha vikwazo kwa wawekezaji vinapatiwa ufumbuzi Ili wafikie malengo ya kuzalisha bidhaa zitakazouzwa ndani na nje ya nchi.
Mwenyekiti wa Kamati hiyo Dk.Joseph Mhagama alieleza hayo jana wakati Kamati hiyo ilipotembelea katika kongani ya kisasa ya Viwanda (Modern Industrial Park) iliyopo Disunyara / Kikongo Mlandizi Wilaya ya Kibaha mkoa wa Pwani.
Amesema ongezeko la uwekezaji hapa nchini limetolana na namna Rais alivyoitangaza nchi sambamba na fursa zilizopo jambo ambalo kimefanya kuwa na wawekezaji wengi wa ndani na nje.
Aidha Kamati hiyo ilimpobgeza mwekezaji wa kongani hiyo ambaye ni mzawa huku ikiahidi kutatua vikwazo allivyoainisha Ili wawekezaji waweze kuwekeza bila vipingamizia na kuwezesha kuwepo kwa maendeleo na kuongeza ajira kwa vijana.
" Tunapopata wawekezaji wa ndani wanaowekeza tunatakiwa kuwawekea mazingira wezeshi Ili waweze kuendana sawa na wawekezaji wa nje na Mwekezaji wa Modern tunaahidi kushirikiana nae kwa kila jambo na kunapotokea tatizo atujulishe tulifanyie kazi kwa haraka," alisisitiza Dk Mhagama.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji Pro. Kitila Mkumbo alimpongeza mwekezaji huyo kwa uwekezaji alioufanya ambapo alisema ameonyesha njia na kuwa mfano wa kuigwa kwa wazawa.
Pro.Mkumbo alieleza kwamba wanaowekeza nchini sio kutoka nje ya nchi pekee wenye bali watanzania nao wameonyesha nia ambapo kwa takwimu za TIC hadi sasa ni asilimia 61 ya wawekezaji Tanzania ambao ni wazawa .
Awali akiwasilisha taarifa ya kongani hiyo Meneja Mauzo na Masoko Turkey estate ambao ni wauzaji wa viwanja vya viwanda katika kongani ya Modern Industrial Park Angela Maingu alisema Mwekezaji wa Kampuni ya Kamaka ya Jijini Dar es Salaam, ndiye aliyewekeza katika kongani hiyo ya kisasa.
Alisema malengo ya Kamaka kuwekeza katika kongani hiyo ni pamoja na kuvutia wawekezaji na teknolojia mpya, kuongeza fursa za kiuchumi pia Kongani hiyo itakuwai kitovu cha utafiti na ugunduzi kwa taasisi za elimu pia kitovu cha mafunzo ya vitendo.
Maingu alisema gharama ya mradi huo hadi kukamilika ikiwa ni pamoja na ujenzi wa viwanda vinavyotarajiwa ni Shilingi 3.5 trilioni.
Kati ya fedha hizo shilingi 1.1 bilioni zitatumika kujenga
miundombinu yote ndani ya kipindi cha miaka mitano na kwamba hadi sasa Shilingi 35 bilioni zimetumika kwa ujenzi wa miundombinu na gharama nyingine zinazohusiana na uwekezaji.
Mradi huo unajengwa katika eneo lenye ukubwa wa ekari za mraba 1,077 ambalo
limegawanywa katika viwanja 210 kati ya hivyo 202 ni kwa ajili ya viwanda, viituo vya umeme viwili maeneo ya biashara mawili, huduma za jamii tatu, bandari kavu
pamoja na mtandao wa barabara za ndani na nje wa kilomita 25.
Maingu pia alisema mpaka kufikia Februari wawekezaji waliotembelea kongani kununua maeneo pamoja na kuonyesha nia ya kuwekeza wanatoka katika nchi za lndia, China, Uturuki, Sudan ya Kusini, Africa ya Kusini, Rwanda, Somalia, Tanzania, Pakistani,
Yemeni, Zambia, Falme za Kiarabu, Misri, Syria, Nigeria, Uganda, Kenya na Canada.
Mradi unajumuisha ujenzi wa miundombinu wezeshi katika utekelezaji wa shughuli za viwanda ambayo inajengwa kwa awamu na kwasasa imefikia asilimia 95.
No comments:
Post a Comment