Ujenzi wa Daraja la Lukuyu kuwaondolea adha wakulima Kata ya Bigwa |
Na Lilian Kasenene,Morogoro
maipacarusha20@gmail.com
Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa TAMISEMI anayesimamia Miundombinu,Mhandisi Rogatus Mativila ameugiza Wakala ya Barabara za Mijini na Vijijini (TARURA) Manispaa ya Morogoro kuhakikisha inakamilisha ujenzi wa daraja la Lukuyu lililopo Kata ya Bigwa ifikapo Agosti mwaka huu
Aidha amesema kukamilika kwa daraja hilo kutawaondolea adha wananchi wa maeneo hayo ya kusafirisha mazao yao ikiwemo mboga mboga ,ndizi kwa kubeba kichwani.
Mhandisi Mativila aliyasema hayo wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa ujenzi wa miundombinu ya barabara inayosimamiwa na Wakala ya Barabara za Mijini na Vijijini (TARURA).
Daraja la Lukuyu litagharimu kiasi cha shilingi milioni 70 na kukamilika kwa ujenzi wa daraja hilo linaenda kuwa mwarobaini kwa wakazi wa kata ya Bigwa.
Pia Naibu katibu mkuu huyo alionyesha kuridhiahwa kwa ujenzi wa barabara ya kichangani iliopo manispaa ya Morogoro iliyogharimu zaidi shilingi milioni 400.
Alisema kwamba kukamilika kwa barabara hiyo itaenda kufungua shughuli za kiuchumi kwa wakazi wa eneo hilo.
“Ni wakati sasa wa wakazi wa eneo hili kunufaika kupitia miundombinu ya Barabara ili kuweza kuwarahisishia mawasiliano na shughuli za usafirishaji,”alisema.
Hata hivyo Mhandisi Mativila
aliwataka TARURA Manispaa ya Morogoro kumalizia kipande cha barabara ya mfungua kinywa kabla ya mvua hazijaanza kunyesha.
Kwa upande wake Meneja wa TARURA Mkoa wa Morogoro Mhandisi Emmanuel Ndyamukama alisema kuwa barabara ya kichangani ni miongoni mwa barabara ambazo zinaenda kuchochea uchumi wa wakazi wa manispaa ya Morogoro kuwa jiji.
Akahaidi kuhakikisha wanatekeleza maagizo yote yaliyotolewa na Naibu katibu mkuu huyo.
No comments:
Post a Comment