RUWASA MANYARA, WATER MISSION KUTUMIA BILIONI 1.5 KUBORESHA HUDUMA ZA MAJI SAFI NA SALAMA VIJIJINI - MAIPAC MEDIA TANZANIA

Breaking

MAIPAC MEDIA TANZANIA

A Centre for Indigenous and Pastoralists Community Informations




Friday 26 July 2024

RUWASA MANYARA, WATER MISSION KUTUMIA BILIONI 1.5 KUBORESHA HUDUMA ZA MAJI SAFI NA SALAMA VIJIJINI

 


Mkuu wa Mkoa wa Manyara Queen Sendiga akihutubia wakati wa uzinduzi wa mradi 






Na Epifania Magingo,Babati 


maipacarusha20@gmail.com


Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira vijijini (RUWASA)Mkoa wa Manyara Chini ya ufadhili wa  Shirika la Misaada la Marekani (USAID)imetia Saini mkataba wa uendelezaji na upimaji ubora na usimamizi wa usalama wa maji ya  kunywa kwa jamii za vijijini ambapo mpango huo utatekelezwa kupitia Mradi wa REAL Water.


Ili kufanikisha Mradi huo RUWASA kwa  kushirikiana na Water Mission  imepokea vifaa vya upimaji wa ubora wa maji kuanzia kwenye chanzo ambapo mradi huo utaanza kutekelezwa katika mkoa wa Manyara kabla ya kusambazwa mikoa mingine hapa nchini.


Mpango wa utafiti Duniani "USAID Water for the World" unaunga mkono juhudi za Serikali ya Tanzania za kuboresha huduma za maji vijini kwa usalama.


Lengo la Mradi huo ni kuchangia maendeleo endelevu kwenye Idara ya Maji ambao utaanza kutekekezwa Chini ya Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira vijijini( RUWASA) Mkoani Manyara.


Akizindua Mradi huo Julai 25,2024  Mkuu wa Mkoa wa Manyara Queen Sendiga amesema kuwa tayari utekelezaji wa mradi huo unapaswa kuanza mara Moja huku akisistiza ufanisi mzuri katika utekelezaji wa mradi huo ili kuweza kunufaisha mikoa mingine hapa nchini.


 Amesema,miradi ya Maji ni muhimu kwa ustawi wa jamii na ameeleza  changamoto kubwa inayoukabili Mkoa huo ni kwamba kuna baadhi ya maeneo ni magumu kufikika ili kutoa huduma ya maji na kudai kuwa vifaa vilivyotolewa vya upimaji wa maji vitasaidia kutatua changamoto hiyo.


Aidha,amesema Serikali imeendelea kutenga fedha kwaajili ya kuongeza mitandao ya Maji kuelekea sehemu ambazo jamii inauhitaji wa maji.


"Changamoto nyingine Mkoa wa Manyara ni Mkoa wa kifugaji ,jamii za kifugaji si unajua ambavo zinakaa,nyumba Moja kule nyingine inakaa baada ya kilomita Moja baada ya kilomita Moja,iyo nayo pekeake  inachangia wananchi walioko mbali kabisa  kusogezewa maji karibu".


Queen Sendiga ameeleza kua Serikali ya Mkoa wa Manyara itaendelea kutoa ushirikiano wa kutosha na kusimamia kuhakikisha kwamba inatekeleza kwa wakati na inaleta matokeo yaliyokusudiwa.


Kiongozi huyo amewaomba Water Mission  kama  wadau  wa maji waendelee kuongeza mtandao wa huduma katika maeneo mengi ndani ya Mkoa wa Manyara ili kuweza kutoa huduma na kwamba Mkoa utahakikisha unaweka mazingira salama ya utekelezaji wa kazi hiyo.


"Leo tumezindua kampeni ambayo inaenda kuanza kufanya kazi kwa Wilaya mbili,nilitamani Wilaya zangu zote Tano ziweze kupata huduma hii muhimu, kwasababu uhakika wa maji safi na salama tunahitaji Mkoa mzima".


Sendiga amesisitiza kuwa vifaa vilivyotolewa katika utekelezaji wa Mradi huo vitumike vizuri na kutunzwa   ili kuleta chachu ya wadau kuleta miradi mingine kwakua upatikani wa maji safi na salama unahitaji huduma nyingi.


Hata hivyo Mkurugenzi wa huduma za Sheria wizara ya Maji Simon Nkanyemka ameomba kuwa mradi huo punde utakapoanza kutekekezwa ni vyema ukashirikisha wataalamu wa Sekta ya Maji ili uweze kufanikiwa na kuleta matokeo mazuri yatakayonufaisha eneo husika na mikoa mingine hapa nchini.


 Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira vijijini ( RUWASA) Injinia Wolta Kirita amesema kuwa,watajitahidi kutoa ushirikiano mzuri kwa kufanya kazi kwa  pamoja na kutao ushauri mzuri wa namna ya kutekelezwa Mradi huo.


Mtaalamu wa Usimamizi wa Miradi ya Maji Safi na Usafi wa  Mazingira kutoka USAID Tanzania Mhandis Francis Mtitu amesema utekelezaji wa mpango wa Mradi huo USAID wa Real Water  Nchini Tanzania utasidia kuimarisha ushirikiano kati Yao na  Serikali,jamii za vijijini na wadau wengine ili kuboresha huduma ya maji na kuhakikisha maji safi ya kunywa yanapatikana kwa vizazi vijavyo.


Naye Mkurugenzi wa Mradi wa Real Water Ranjiv Khush amesema Mradi huo unafanya utafiti kwenye nchi kumi na mbili ikiwemo Tanzania na kwamba  utahakikisha kuwa hautakosa fedha za upimaji wa ubora wa maji kutoka kwenye jamii punde watakapoanza zoezi la upimaji wa maji.


"Kutokana na matokeo ambayo tutaweza kuyapata wa ufaulu wa ubora wa maji tutaweza kwenda kwenye mikoa mingine ya nchi ya Tanzania kwaajili ya kwenda kufanya kazi".


Mradi huo wenye gharama dola 697,355  na utadumu kwa muda wa miaka mitano ambao utaanza kutekelezwa katika Wilaya mbili za Hanang na Mbulu Mkoani Manyara.


Mwisho


No comments: