Kamanda wa polisi mkoa wa Morogoro Alex Mkama
Na Lilian Kasenene,Morogoro
maipacarusha20@gmail.com
WANAWAKE wawili wanashikiliwa na Jeshi la Polisi Wilaya ya Gairo, mkoani Morogoro kwa madai ya unyang'anyi wa Pikipiki na fedha kwa kutumia silaha ya jadi aina ya nondo pamoja na panga.
Wanawake hao ni Farida Msafiri Charles (26) Mkulima mkazi wa mtaa wa Uchagani Gairo na Grace Robert Chiduo (24) Mkulima mkazi wa kitongoji cha Sambweti Gairo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro SACP Alex Mkama alisema tukio hilo lilitokea Agosti 13, 2024 saa 12 jioni ambapo wanawake hao walimkodi muendesha pikipiki ya abiria (bodaboda) Ndoni Ndumwa John (32) Mkazi wa kitongoji Kichangani Wilaya ya Kiteto Mkoa wa Manyara.
Alisema John akiwa na pikipiki yake yenye namba MC 936 DRZ aina ya Houjue nyeusi, kutoka kijiweni kwake Sunya Kiteto Manyara wanawake hao walimtaka awapeleke Sambweti Gairo.
Alisema wakiwa njiani kuelekea Sambweti Gairo, wanawake hao walimvamia kwa ushirikiano na vijana wengine wakiume wawili ambao walitokea vichakani na kumshambulia kwa panga sehemu mbalimbali za mwili wake kisha kumnyang'anya pikipiki na Shilingi 4000.
Baada ya kuripotiwa kwa tukio hilo Jeshi la Polisi Wilaya ya Gairo kwa kushirikiana na Kiteto lilifanya msako mkali wa Watuhumiwa haonl na kuwakamata wanawake hao wakiwa na Pikipiki hiyo pamoja na fedha.
Aidha Watuhumiwa wanashikiliwa katika kituo cha Polisi Gairo kwa mahojiano na watafikishwa Mahakamani kwa hatua zaidi za kisheria.
....
No comments:
Post a Comment