![]() |
| RAIS SAMIA Suluhu Hassan |
![]() |
| Wanafunzi WA shule ya Msingi Makao wakipata chakula Cha mchana kinachotolewa na FCF |
Mussa Juma,Maipac
maipacarusha@gmail.com
Meatu. Serikali na Taasisi ya Friedkin Conservation Fund (FCF) ambayo imewekeza shughuli za Utalii, wilayani Meatu, mkoa wa Simiyu, wamepongezwa kuendeleza miradi ya Afya na elimu kwa manufaa makubwa katika wilaya hiyo.
Wakati serikali ikiongeza fedha za elimu, Afya na barabara katika wilaya hiyo pia FCF imekuwa na mradi wa kutoa chakula bure shuleni, kufadhili wanafunzi katika masomo yao, mradi ya ujenzi nyumba sekta za afya na vituo vya kupambana na wanyama wakali ikiwepo Tembo.
Katika ziara ya Rais Samia Suluhu, katika wilaya hiyo, alisema serikali itaendelea kuboresha sekta za Afya, Elimu, Maji, Barabara na kilimo hasa cha Pamba katika wilaya hiyo.
Waziri wa nchi ofisi ya Rais (TAMISEMI), Mohamed Mchengerwa alieleza serikali imejenga shule mpya nne za sekondari na shule mbili za msingi mkoa Simiyu huku ikitoa zaidi ya sh 8.4 bilioni sekta ya afya wilaya hiyo ya Meatu.
Alisema Serikali pia imeongeza bajeti ya barabara katika wilaya hiyo ya Meatu , kutoka billioni 1 mwaka 2021/2022 hadi kufikia bilioni 4 mwaka 2023/24
Mwenyekiti wa halmashauri ya Meatu, Anthony Philipo akizungumzia na mwandishi wa habari hizi kuhusiana maendeleo ya sekta ya elimu katika wilaya hiyo, alipongeza serikali na wawekezaji FCF kupitia Mwiba Holding Ltd kwa mchango wao
Alisema kuna ushirikiano mkubwa baina ya halmashauri ya Meatu na Wawekezaji hao, katika kusaidia jamii, ikiwepo kudhibiti tembo kuharibu mali za wananchi.
Akizungumzia utoaji bure wa chakula katika shule ya msingi Makao, Mwenyekiti huyo alisema mradi huo umekuwa na faida kubwa.
"Mradi unaendelea vizuri sana, hatuna shida na mwekezaji kwani anaendelea kutoa chakula na sasa idadi ya wanafunzi imeongezeka shuleni na utoro umepungua"alisema
Philipo pia alisema katika wilaya hiyo, kulikuwa na migogoro baina ya Tembo na wananchi na sasa imepungua kutokana na Tembo kufungwa mikanda ya kielektroniki (GPS Collar) ya kuwadhibiti kuingia katika mashamba na makazi ya watu na kujengwa vituo vya kudhibiti tembo.
Meneja miradi wa Taasisi ya Friedkin Conservation Fund(FCF) Aurelia Mtui alisema wamefanikiwa kufunga mikanda ya kielekroniki (collar) kwa Tembo 10 katika eneo la Ranchi ya Mwibai lililogharimu Sh 232 milioni ili kutatua migogoro na jamii, alisema taasisi hiyo imeongeza fedha za kusaidia Jamii.
MWISHO




No comments:
Post a Comment