![]() |
| Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mzuri Africa, Shabani Mgonja |
Lilian Kasenene, Morogoro
maipacarusha20@gmail.com
WAKULIMA wametakiwa kukumbatia matumizi ya teknolojia na zana za kisasa za kilimo ili kuongeza tija, kuboresha uzalishaji wa mazao na kuzalisha mazao yanayokidhi viwango vya soko la kimataifa.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mzuri Africa, Shabani Mgonja, alitoa wito huo wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya Nanenane Kanda ya Mashariki yanayoendelea mkoani Morogoro.
Maonyesho hayo yanahusisha mikoa ya Morogoro, Dar es Salaam, Pwani na Tanga.
Mgonja alisema teknolojia ya Mzuri Africa kwa sasa inatumika katika zaidi ya nchi 50 duniani, huku Tanzania ikiwa makao makuu ya teknolojia hiyo kwa Bara la Afrika.
Alisema lengo la kuanzishwa kwa teknolojia hiyo ni kubadili mtazamo wa wakulima, ili waache kujiona wanyonge na kubaki kuwa wakulima wadogo, badala yake watumie teknolojia kuongeza uzalishaji na kukuza shughuli zao za kilimo.
> "Nia na madhumuni ya kuanzishwa kwa teknolojia hii ni kubadilisha mitazamo ya wakulima kujiona wanyonge na kubaki kuwa wakulima wadogo, jambo ambalo si sahihi," alisema Mgonja.
Aidha, alieleza kuwa matumizi ya zana na teknolojia za kisasa yatamwezesha mkulima kulima maeneo makubwa kwa muda mfupi, kuongeza uzalishaji, kuwa mkulima wa kiwango kikubwa na kuona kilimo kama biashara yenye tija badala ya kukikimbia.
Mwisho.



No comments:
Post a Comment