Mahakama ya Afrika ya Haki za Binaadamu "yalia "Nchi kupuuza hukumu zake - MAIPAC MEDIA TANZANIA

Breaking

MAIPAC MEDIA TANZANIA

A Centre for Indigenous and Pastoralists Community Informations




Monday 20 February 2023

Mahakama ya Afrika ya Haki za Binaadamu "yalia "Nchi kupuuza hukumu zake

 



Mwandishi wetu, Maipac

maipacarusha20@gmail.com


Arusha.Nchi wanachama wa Umoja wa Afrika(AU) zimeombwa kutekeleza hukumu   zinazoatolewa na Mahakama ya Afrika ya Haki za Binaadamu na Watu(AFCHPR) Ili kuendeleza misingi ya Haki za binaadamu katika nchi wanachama.



Mahakama hiyo ilianzishwa mwaka 2004  kutokana na maazimio ya  Umoja wa Afrika ya mwaka 1998, Makao makuu yake yapo jijini Arusha,hata hivyo, imekuwa na changamoto ya nchi kadhaa wanachama wa umoja wa Afrika(AU) kutotekeleza hukumu ambazo zimekuwa zikitolewa.



 Rais wa mahakama hiyo, Jaji Imani  Aboud akizungumza  katika ufunguzi wa mwaka wa mahakama hiyo Leo February 20,2023 jijini Arusha , amesema bado nchi nyingi  katika hazitekelezi hukumu za Mahakama hiyo .


Amesema mahakama hiyo ipo kisheria na imeundwa na AU na kwa mujibu wa mkataba wa AU ibara ya 30 nchi wanachama zinapaswa kuheshimu maamuzi ya mahakama hiyo.


Jaji Iman amesema tangu mahakama hiyo ilipoanzishwa miaka 16 iliyopita imeweza kutoa hukumu katika mashauri zaidi ya 200 ambayo yalifikishwa kutoka nchi mbalimbali


" changamoto iliyopo ni baadhi ya nchi kutotekeleza baadhi ya hukumu ambazo zimekuwa zikitolewa na mahakama hii "amesema 



Akizungumza katika hotuba ya  ufunguzi wa  mwaka wa mahakama  hiyo, 2023 Makamu wa Rais wa Jamuhuri  ya Muungano Dk Philip  Mpango amesema, Serikali ya Tanzania inatambua umuhimu wa mahakama hiyo na itaendelea kufanya nayo kazi .


Hata hivyo, amesema kumekuwepo na changamoto kadhaa katika utekelezwaji wa hukumu za mahakama hiyo na akashauri mahakama kuboresha mahusiano na mahakama za ndani ya nchi, ili kuondoa dhana  kuwa  mahakama hiyo kuingilia uhuru wa mahakama za ndani.


Amesema  ni muhimu kuwepo na ushirikiano na mafunzo baina ya watendaji wa mahakama  majaji, Mawakili na mahakimu juu ya masuala ya haki za binaadamu .



Kauli mbiu ya mwaka wa mahakama hiyo mwaka huu ni "kuunganisha mifumo wa sheria za haki za binaadamu za kikanda na kimataifa katika mifumo ya kitaifa" 


Awali Rais wa mahakama ya Afrika ya Mashariki Jaji  Nestor Kayobera  na Rais wa bunge la  Afrika, Fortune Charumbira walieleza kuridhishwa na kazi nzuri ambayo inaendelea kufanya na mahakama hiyo katika kulinda na kutetea na haki za binaadamu barani Afrika.


Katika ufunguzi wa shughuli za Mahakama hiyo,pia wamehudhuria majaji wa mahakama za ndani ya nje,majaji wa mahakama ya Afrika ya Mashariki, Mawakili, wawakilishi wa mashirika ya kutetea haki za binaadamu na viongozi wa Serikali ngazi mbalimbali akiwepo Waziri wa Katiba na Sheria Dk Damas Ndumbaro.


No comments: