WALIMU MKAPA SEKONDARI WAPONGEZWA KWA KUFAULISHA VIZURI WANAFUNZI - MAIPAC MEDIA TANZANIA

Breaking

MAIPAC MEDIA TANZANIA

A Centre for Indigenous and Pastoralists Community Informations




Thursday 16 February 2023

WALIMU MKAPA SEKONDARI WAPONGEZWA KWA KUFAULISHA VIZURI WANAFUNZI

 Na Mwanadishi wetu, Mirerani
maipacarusha20@gmail.com


WAJUMBE wa Baraza la Mamlaka ya Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, wamechangia sh20,000 kila mmoja ili kuwapongeza na kuwafanyia sherehe walimu wa sekondari ya Mirerani B.W. Mkapa kwa kufaulisha vyema wanafunzi wa kidato cha nne.

Wajumbe wa mamlaka hiyo wamechanga kiasi cha sh20,000 kila mmoja ili kuwezesha sherehe ya kuwapongeza walimu wa shule ya sekondari Mirerani B.W. Mkapa itakayofanyika mwishoni mwa mwezi huu.

Diwani wa kata ya Endiamtu, Lucas Zacharia akizungumza kwenye kikao cha baraza la mamlaka hiyo amesema walimu wa shule hiyo wanapaswa kupongezwa ili kuungwa mkono.

Zacharia amesema walimu wa shule hiyo wamejitahidi mno kuhakikisha wanafunzi wanafanya vyema kwani hata masomo ya hesabu na sayansi yaliyozoeleka ni magumu, wamefaulu.

“Walimu wamejitahidi mno kwani hakuna daraja sifuri, wanafunzi 13 wamepata daraja la kwanza, wanafunzi 42 daraja la pili, wanafunzi 61 daraja la tatu na 43 daraja la nne,” amesema.

Mwenyekiti wa mamlaka ya mji mdogo wa Mirerani, Adam Kobelo amesema wajumbe wameridhia kuchanga kwanza fedha zao wenyewe kisha wadau wengine nao watafuatwa.

“Tutaunda kamati maalum ambayo itafanikisha sherehe ya kuwapongeza walimu ili mwaka huu tena wawafundishe vyema watoto wetu na mwakani wafaulu zaidi,” almesema Kobelo.

Diwani wa kata ya Mirerani Salome Nelson Mnyawi amesema walimu hao wanastahili kupongezwa kwani wameipa sifa Mirerani kutokana na ufaulu huo wa wanafunzi wa kidato cha nne.

Amesema anatarajia walimu hao hawatabweteka ila wataongeza juhudi katika kufundisha ili watoto wa mji wa Mirerani wapige hatua kubwa kwenye suala la elimu na taaluma kwa ujumla.

Mjumbe wa bodi ya shule hiyo Jema Lilama amepongeza hatua hiyo ya viongozi hao kuandaa sherehe kwa ajili ya kuwapa mkono wa shukrani walimu wa shule hiyo.

“Shule hii inazidi kutupa heshima kwenye mji wetu wa Mirerani kwani watoto wetu watakuja kuwa wataalam kwenye miaka ijayo na kusaidia jamii,” amesema Jema.

Mwenyekiti wa kitongoji cha Tanesco, Justin Abraham amesema walimu hao wamewatoa kimasomaso wananchi wa mji mdogo wa Mirerani kutokana na matokeo hayo ya kidato cha nne.

"Mara ya kwanza walifanikisha mwanafunzi mmoja kuchaguliwa kwenda kidato cha tano shule ya sekondari Tabora boys, leo wametokomeza ziro wanastahili kupongezwa kwa kweli," amesema.



No comments: