NGOs ARUSHA ZAUNDA MTANDAO WA KUKABILIANA NA UKATILI DHIDI YA WANAWAKE NA WATOTO WA JAMII ZA PEMBEZONI - MAIPAC MEDIA TANZANIA

Breaking

MAIPAC MEDIA TANZANIA

A Centre for Indigenous and Pastoralists Community Informations




Thursday, 6 July 2023

NGOs ARUSHA ZAUNDA MTANDAO WA KUKABILIANA NA UKATILI DHIDI YA WANAWAKE NA WATOTO WA JAMII ZA PEMBEZONI

 

Mkurugenzi mtendaji wa Mimutie women Organization Rose Njilo akielezea dhamira ya mtandao WA kupinga ukatili wa jinsia kwa jamii za pembezoni 



 

NA: Andrea Ngobole, Arusha


maipacarusha20@gmail.com


Mashirika yasiyo ya kiserikali mkoa wa Arusha, yameunda mtandao wa kukabiliana na matukio ya ukatili dhidi ya wanawake na watoto kwa jamii za pembezoni.

Mtandao huo, unatarajiwa kujihusisha na kutoa elimu kupinga ukatili dhidi ya wanawake na watoto, kufanya utafiti wa kukomesha ukatili, kuwaokoa watoto waliofanyiwa ukatili na kuuganisha mashirika hayo na wadau wengine wa ndani na nje ya nchi katika kukabiliana na ukatili kwa wanawake na watoto.




Afisa Maendeleo Mkoa wa ARUSHA Blandina Nkini akizungumza Katika uzinduzi WA mtandao huo

Akizungumza katika uzinduzi wa mtandao huo, Afisa maendeleo mkoa wa Arusha Blandina Nkini alipongeza Mashirika yasiyo ya kiserikali mkoa Arusha yakiongozwa na Mimutie women Organization kuungana kupambana na ukatili wa jinsia ambao unaongezeka kwa kasi nchini.

Ameutaka mtandao huo kuongeza Katika majukumu yao kuwa na mpango wa elimu ya kumlinda mtoto wa kiume asitendewe vitendo vibaya ili kujenga Taifa imara kwani kuwasahau watoto wa kiume kunapelekea kuwa na kizazi kisichojitegemea.

 

Mkurugenzi mtendaji wa shirika la Mimutie Women Organization Rose Njillo amesema kuwa mtandao huo unaoundwa na mashirika 10 ya utetezi wa haki za jamii za pembezoni utakuwa chachu ya kufikia malengo ya kupinga ukatili wa kijinsia hususani ndoa za utotoni na za lazima, ukeketaji kwa watoto wa kike, vipigo ndani ya ndoa na elimu ya afya ya uzazi kwa wanawake na wasichana wa jamii za pembezoni.

 

“Sisi Mimutie Women Organization tumejitahidi sana kupaza sauti za kupinga ukatili wa jinsia kwa jamii za pembezoni kwa miaka kumi sasa na ndiyo maana tumeona ni vema sasa kuunda mtandao wa kupinga ukatili huu kwa jamii hizi ili kuwa na sauti pana Zaidi kwa kushirikiana na mashirika mengine 10 yenye mlengo wa kutetea haki za jamii za pembezoni, naamini kwa pamoja tutafikia malengo ya kutokomeza ukatili huu kabisa.” Alisema mkurugenzi huyo

 

Mwenyekiti wa UWT Arusha Flora Zelothe akizungumza na Waandishi wa Habari mara baada ya kuzinduliwa KWA mtandao huo

Mwenyekiti wa umoja wa wanawake Tanzania (UWT) Mkoa wa Arusha Flora Zelothe amewapongeza Mimutie Women Organization na mashirika mengine kumi kuanzisha mtandao huo wa kupinga ukatili wa kijinsia kwa jamii za pembezoni na kuwataka kushirikiana na Mtakua iliyoanzishwa na serikali ya awamu ya sita katika kupata taarifa kamili za matendo ya ukatili kwa jamii kuanzia ngazi ya kitongoji na vijiji ili kupunguza ukatili wa jinsia kufikia asilimia sifuri Mkoani Arusha.

“Nawapongeza sana mashirikia yasiyo ya serikali mkoani Arusha mnafanya kazi nzuri na kwa kuwa mmeanzisha mtandao huu basi mtakuwa na sauti pana zaidi ya kusemea madhara ya ukatili wa jinsia, ukatili kwa watoto na wanawake ili uweze kwisha kabisa mkoani Arusha”. Alisema


Mkurugenzi wa ANGONET Petro Aham amesema wanafurahi kushirikishwa na mtandao huu unaoanza kufanya kazi katika mkoa wa Arusha na kuahidi kusaidia kuweka mpango mkakati wa kufichua na kupinga ukatili wa kijinsia ili  kuhakikisha kunakuwa na jamii za pembezoni inayotambua na kuheshimu haki za binadamu.

 

Mkurugenzi wa shirika la wanahabari la kusaidia jamii za pembezoni la MAIPAC, ambao ni miongoni mwa waanzilishi wa mtandao huo, Mussa Juma alisema lengo kubwa la mtandao ni kusaidia jamii za pembezoni kukabiliana na ukatili.

Maipac tumekuwa na miradi kadhaa kusaidia jamii hii ikiwepo wa mazingira unaodhaminiwa na mfuko wa mazingira duniani (GEF) kupitia miradi midogo ya shirika la maendeleo la umoja wa mataifa (UNDP) na karibuni tumekuwa na mradi wa kupambana na ukeketaji wilaya ya Longido ambao unadhaminiwa na marafiki wetu wa nchini Canada sasa kupitia mtandao tutafanya kazi kubwa kwa kushirikiana na mashirika mengine” alisema

Jopha Malulu mkazi WA Mundarara Wilayani Longido


Naye Jopha Malulu mama wa watoto watatu, Mhanga wa ndoa za utotoni anasema kuanzishwa kwa mtandao huu utasaidia sana kupunguza ukatili kwa mtoto wa kike kuozeshwa akiwa bado mdogo, vipigo ndani ya ndoa na kunyimwa haki ya kupata elimu ili aweze kufikia malengo makubwa kwa watoto wa kike na kupunguza umaskini kwa jamii hizo.

 “Niliolewa nikiwa na miaka 14 bila ridhaa yangu ila kwa mapendekezo ya wazazi wangu nikiwa sielewi masuala ya ndoa jinsinya kumhudumia Mume na baadae baada ya kujitambua na kupigania haki zangu niliachana na Mume wangu na kunyimwa hata sehemu ya kuishi n ahata kuwaona watoto wangu wawili niliopata na Mume wangu.” Alisema

 

No comments: