UCHAGUZI WA MAKAMU MWENYEKITI SIMANJIRO WASHINDWA KUFANYIKA KWA MARA YA TATU - MAIPAC MEDIA TANZANIA

Breaking

MAIPAC MEDIA TANZANIA

A Centre for Indigenous and Pastoralists Community Informations




Thursday, 6 July 2023

UCHAGUZI WA MAKAMU MWENYEKITI SIMANJIRO WASHINDWA KUFANYIKA KWA MARA YA TATU

 

Mbunge wa Jimbo la Simanjiro Christopher Ole Sendeka na baadhi ya madiwani wamegomea uchaguzi huo wakitaka madiwani saba waliochukua fomu wapigiwe kura badala ya majina ya madiwani watatu yaliyorudishwa na CCM mkoa


 


Na Mwandishi wetu, Simanjiro


maipacarusha20@gmail.com


UCHAGUZI wa Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara, kupitia CCM umeshindwa kufanyika kwa mara ya tatu.


Mbunge wa Simanjiro Christopher Ole Sendeka na baadhi ya madiwani wamegomea uchaguzi huo wakipinga kukatwa majina ya madiwani wanne walioomba nafasi hiyo.


Katibu wa CCM Wilaya ya Simanjiro, Amos Shimba amethibitishwa kutofanyika kwa uchaguzi huo wa kumpata makamu Mwenyekiti kupitia CCM.


"Ni kweli uchaguzi wa kumpata makamu umevurugika hivyo haujafanyika ila tumeshatuma taarifa kwenye ngazi ya juu yetu kwa hatua zaidi subirini majawabu," amesema Shimba.


Ole Sendeka akizungumza kwenye kikao hicho cha uchaguzi kilichofanyika kwenye ofisi ya CCM wilaya hiyo alipinga kupigiwa kura  kwa majina ya madiwani watatu yaliosomwa na Shimba akidai anataka majina yote saba.


"Wagombea walikuwa saba, walichukua fomu na kurejesha, tunataka majina yao yatajwe ili tuwapigie kura na siyo majina hayo ya madiwani watatu mliyotusomea hapa," amesema Ole Sendeka.


Shimba akisoma majina hayo matatu kwenye kikao hicho yaliyoidhinishwa na kamati ya siasa ya mkoa na kata zao kwenye mabano ni Albert Msole (Ngorika), Lucas Zacharia (Endiamtu) na Kaleiya Mollel (Msitu wa Tembo).


"Mbunge wewe ni mjumbe wa kamati ya siasa ya wilaya na ulikuwepo kwenye kikao Mirerani tulichopitisha majina haya matatu inakuweje leo unapinga majina haya?" amehoji Shimba.


Kutokana na hali hiyo Mwenyekiti wa halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro, Baraka Kanunga akafunga kikao hicho cha uchaguzi, hivyo kutopigwa kura kwa madiwani hao watatu.


Halmashauri sita za mkoa wa Manyara, zimeshafanya uchaguzi wa Makamu Mwenyekiti ila Simanjiro pekee ndiyo bado kizungumkuti kimetanda kwenye nafasi hiyo.



No comments: