NJAA INAVYOSABABISHA UTORO KWA WANAFUNZI WA SHULE ZA MSINGI WILAYANI LONGIDO - MAIPAC MEDIA TANZANIA

Breaking

MAIPAC MEDIA TANZANIA

A Centre for Indigenous and Pastoralists Community Informations




Thursday, 6 July 2023

NJAA INAVYOSABABISHA UTORO KWA WANAFUNZI WA SHULE ZA MSINGI WILAYANI LONGIDO


 

Baadhi ya wanafunzi wa sule ya Msingi Orbomba wakibadilishana mawazo nje ya madarasa yao wakati wa mapumziko ya mchana


Baadhi ya wanafunzi wa shule ya Msingi Orbomba wakiwa mapumziko 

NA: Andrea Ngobole, Longido

 

maipacarusha20@gmail.com

 


Kati ya watoto kumi wa shule ya Msingi Orbomba wilayani Longido Mkoani Arusha ni watoto sita tu ambao hufika shule na kuhudhuria masomo. Hii ni asilimia arobaini ya watoto wote wanaotakiwa kufika shule. Njaa imesababisha wanafunzi washindwe kuhudhuria masomo. 

 

Hali iliyopo katika shule hii ndiyo picha halisi iliyopo katika shule za msingi 43 zilizopo wilayani Longido. Vijiji vingi vya wilaya ya Longido vinakabiliwa na ukame ambao umeleta njaa kali katika familia kiasi kwamba watoto wanashindwa kwenda shule.

 

Mwalimu Lekishon Thomas wa Shule ya Msingi Orbomba anakiri utoro wa wanafunzi shuleni hapo unaosababishwa na njaa kali. Hata wale wachache wanaohudhuria masomo, utendaji wao darasani siyo mzuri kwasababu ya njaa. Kuna baadhi wanahudhuria masomo asubuhi tu, ikifika mchana hushindwa kuvumilia njaa na kutoroka.

 “Kimsingi mahudhurio ya watoto shuleni hapa ni madogo kutokana na njaa, walimu pia tunashindwa kuendelea na vipindi vya mchana kwani usikivu na uelewa wa watoto unakuwa mdogo sana kwa sababu ya njaa,” anasema 

Anasema kamati ya shule imepanga kutafuta chakula kwa wahisani ili waanze kuwapikia wanafunzi hao na baaadae wazazi waje wachange shilingi 18,000 kwa muhula ili waendelee na utaratibu wa kuwapikia chakula. 

Shule hiyo ina jumla ya wanafunzi 445 ambapo mahudhurio ni wastani wa asilimia 60 na asilimia 40 hawahudhurii shule kabisa kutokana na njaa.

Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Ngoswaki Bi. Kwamboka Nyanami naye anakiri kuwa tatizo la njaa linasababisha utoro kwa wanafunzi wa shule hiyo pia inayopatikana katika Kata ya Engarenaibor wilayani hapo.

 

Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msing Kimokowa, Robert Minja anaainisha changamoto kubwa ya utoro wa wanafunzi shuleni hapo inasabishwa na njaa. Anaeleza kuwa wazazi pia wana mwamko mdogo katika kuchangia chakula kwa wanafunzi.

 

Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Ketumbeine Felix Mungaya amesema njaa ilisababisha sana utoro wa wanafunzi shuleni hapo na baada ya kugundua hilo waliomba mashirika yasiyo ya serikali kutoa msaada wa chakula shuleni hapo na kuanza kupika chakula cha mchana na kupelekea utoro kupungua kwa kiasi kikubwa na kuongeza tija katika ufundishaji na kuongeza ufaulu wa wanafunzi.

 

Aidha uchunguzi uliofanywa na chombo hiki wilayani hapo umebaini kuwa baadhi ya watoto wanaosoma katika shule hizo hulazimika kwenda mjini Longido na wengine hadi Arusha mjini kuomba chakula kwa wasamaria wema ili waweze kupeleka nyumbani kwa ajili ya mlo wa familia.

 

Kwa mujibu wa Sera ya Lishe Bora nchini Tanzania ya Mwaka 1992 lishe ni mchakato wa chakula mwilini na  kila mwanadamu anapaswa kuzingatia makundi matano ya chakula ya nafaka, matunda, mbogamboga, nyama na mafuta ili kuepukana na utapiamlo.      

Wadau wa elimu mkoani Arusha wanashauri kwamba ili mwanafunzi aweze kusoma na kufaulu vizuri ni lazima asiwe na changamoto ya njaa kwani pia upatikanaji wa lishe bora na salama kwa matumizi ya wanadamu ni moja ya huduma za lazima kwa maisha na ustawi wa wanadamu.

Katibu wa Jumuiya ya Wamiliki wa Shule na Vyuo Binafsi mkoani Arusha (TAMNGOSE) Malias Mollel anakiri kuwa njaa inaweza kusababisha utoro kwa wanafunzi na kusababisha ufaulu mdogo na kusisitiza kuwepo utaraibu wa upatikanaji wa chakula cha mchana shuleni ambao utasaidia kuondoa tatizo la utoro kwa wanafunzi.

Afisa Elimu Msingi Wilaya ya Longido, Deusdedit Bimbalirwa amekiri kumekuwepo na utoro katika shule za msingi kutokana na tatizo la njaa.

Bimbalirwa alisema kuna baadhi ya wanafunzi wameondoka na wazazi wao kwenda kutafuta malisho ya mifugo.

" Kwa kawaida ukame unapokuwa mkali jamii za wafugaji huhama na mifugo sasa na wanafunzi wanahama nao," alisema.

 

Alieleza kuwa pia kutokana na njaa wanafunzi wanapungua madarasani na kurudi majumbani.


Anasema Halmashauri ya Longido imeanza kulifanyiakazi tatizo hilo kwa kupeleka mashuleni na vijijini chakula cha msaada na bei nafuu.


"Tayari chakula cha msaada kimeanza kupelekwa mashuleni lakini pia chakula cha bei nafuu ili kukabiliana na hali hii" alisema 

Mahindi ya bei nafuu yaliyopelekwa na serikali yanauzwa kwa shilingi elfu themanini (80,000/=) kwa gunia. Hata hivyo, wananchi wanashindwa kununua kwa sababu ya kipato duni kwani masharti ya serikali ni kuuza kwa gunia na siyo kwa debe moja.


Bei ya mahindi katika soko la Longido ni shilingi 135,000 kwa gunia na bei ya debe moja la mahindi linauzwa kati ya shilingi 24000/= mpaka 30000/= ambapo kama serikali ingeuza mahindi yake kwa debe moja wangeuza kwa shilingi 16,000/=

 Kutokana na uhaba wa chakula unaokabili familia nyingi wilayani hapa, baadhi ya mashirika yasiyo ya kiserikali yanayotekeleza miradi kudhibiti athari za mabadiliko ya tabianchi katika wilaya hii ya Longido yameanza kusambaza chakula cha bure kwa kaya zilizokumbwa na njaa.

 

Shirika la Utafiti, Maendeleo na Huduma kwa Jamii (CORDS) limekabidhi tani 7.1 za mahindi kwa kaya 395 za vijiji viwili vya Ildonyo na Orpukeli ambapo kaya 165 za kijiji cha Ildonyo zilipatiwa msaada wa chakula hicho na kijiji cha Orpukeli kaya 230 ambapo kila kaya ilipatiwa kg 20 za mahindi ili kukabiliana na uhaba wa chakula.

 

Akizungumza wakati wa ugawaji mahindi hayo, afisa idara ya miradi ya shirika la CORDS, Charles Dominick alisema wameamua kutoa mahindi ya msaada baada ya kubaini kaya nyingi zinakabiliwa na njaa kali kiasi kwamba watoto wanashindwa kwenda shule.

 

Kaimu Afisa Kilimo wa wilaya ya Longido, Mariam Fivawo anasema ukame umesabisha uhaba wa chakula katika maeneo mengi ya wilaya hiyo ambayo asilimia 95 ya wananchi wake ni wafugaji.

No comments: