Wazazi watakiwa kuwapa watoto uhuru wa kujieleza. - MAIPAC MEDIA TANZANIA

Breaking

MAIPAC MEDIA TANZANIA

A Centre for Indigenous and Pastoralists Community Informations




Friday, 28 July 2023

Wazazi watakiwa kuwapa watoto uhuru wa kujieleza.


Salha Ramadhani mkazi wa Mrombo jijini Arusha akizungumza na Maipac Media Tanzania juu ya umuhimu wa kujieleza kwa mtoto wa kike

Mwanasheria Christina Israel wa ofisi ya mawakili ya Tech. Advocates iliyopo kwa mrombo jijini Arusha akizungumza na Maipac Media Tanzania ofisini kwake mapema leo


 NA: BEATRICE MCHOMVU, FJS

 

maipacarusha20@gmail.com

Wazazi nchini wametakiwa kuwapa watoto wao haki na uhuru wa kujieleza ili kupunguza matendo ya Ukatili wanayotendewa na ndugu au jamaa zao majumbani na shuleni.

 

Uhuru wa kujieleza kwa mtoto utapelekea wazazi kufahamu madhila wanayokutana nayo watoto wawapo majumbani na mashuleni na hivyo kupunguza ukiukwaji wa haki za watoto na hivyo kutengeneza jamii inayoheshimu haki za mtoto.


Christina Israel, mwanasheria kutoka ofisi ya Tech. Advocates amesema hayo leo July 28 ofisini kwake alipokuwa akizungumza na Maipac media Tanzania, kuwa kumpa mtoto haki ya kujieleza sio malezi mabaya na kulingana na sheria ya mwaka 2019 kifungu cha 11 kinasema mtoto ana haki ya kutoa maoni yake.

 

Amesema kuwa kutompa mtoto haki ya kujieleza ni kosa la jinahi na adhabu yake ni kulipa faini isiyozidi shillingi million 5 au kifungo kisichozidi miezi 6 au vyote kwa pamoja kutokana na kifungu cha 14 cha Sheria za watoto.

 

Amewashauri wazazi wawape watoto wao nafasi ya kujieleza kwa sababu ni haki kisheria na itawasaidia kujua kama kuna haki zao zimevunjwa au kufanyiwa ukatili na hivyo kuwa rahisi kutatua changamoto zao.


Amesema kuwa uhuru wa kujieleza kwa mtoto yoyote ndiyo msingi thabiti wa kufahamu matendo maovu wanayotendewa watoto na hivyo kupunguza ama kuondoa madhara hayo kwa watoto.

 

Wilton Harrison (19) mkazi wa kwa mrombo jijini Arusha anasema anashukuru wazazi wake walimpa nafasi ya kujieleza toka akiwa mtoto mdogo na hivyo ilikuwa rahisi kwake kuwaeleza changamoto zozote anazokutana nazo na kutatuliwa na wazazi wake ila pia imempa nafasi ya kujiamini anaapozungumza mbele ya watu.

 

Amesema kuwa ni muhimu watoto kusikilizwa kwa sababu ni haki yao ya msingi toka kuzaliwa kwao na ndiyo njia pekee ya kusikilisizwa na wanafamilia wengine ili kutatuliwa changamoto zao.

 

Mama Safina akiwa dukani kwake amesema haki ya kujieleza kwa mtoto ni muhimu kwa kukuza ufahamu wake

 

Kwa upande wake Mama safina mkazi wa kwa mrombo na mfanyabiashara wa nafaka katika soko la kwa mrombo, amesema kuwa ni muhimu kuwasikiliza watoto ili kujua wanachokitaka na kufanyia kazi mawazo yao kwa sababu watoto Wana mawazo makubwa na mazuri.

 

Reginald Mallya (45) mkazi wa Murieti jijini Arusha na Baba wa watoto watatu amesema kwa upande wake ni muhimu kuwasikiliza na kuwapa watoto uhuru wa kuongea na kutendea kazi mawazo yao yanaweza kuwa mazuri au mabaya ili wawaelimishe lipi ni wazo zuri ama wazo baya.

 


Reginald Mallya mkazi wa Murieti jijini Arusha amesema kuwapa uhuru wa kujiel;eza watoto kunasaidia kupunguza ukatili kwa watoto majumbani

 

Wilton Harrison (19) mkazi wa kwa mrombo jijini Arusha anashukuru wazazi wake kwa kumpa uhuru wa kujieleza unaomsaidia sasa kupambana na mazingira ya kazi zake

No comments: