Waziri Mchengerwa atoa maagizo mazito Kamati Ugawaji vitalu vya uwindaji - MAIPAC MEDIA TANZANIA

Breaking

MAIPAC MEDIA TANZANIA

A Centre for Indigenous and Pastoralists Community Informations




Friday, 14 July 2023

Waziri Mchengerwa atoa maagizo mazito Kamati Ugawaji vitalu vya uwindaji

  

Waziri wa Maliasili na Utalii Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa 




Na: Mwandishi wetu,Arusha

maipacarusha20@gmail.com


Waziri wa Maliasili na Utalii, Mohamed Mchengerwa amezindua Kamati ya Ushauri ya Ugawaji wa Vitalu vya Uwindaji wa Kitalii nchini   na kuipa majukumu  kurekebisha kasoro zote zilizojitokeza katika sekta hiyo.


Sekta ya Uwindaji wa Kitalii ambayo ilikuwa imefifia Sasa imeanza kuimarika na mapato kwa mwaka yamefikia bilioni 30 na Sasa yanatakiwa kuongezeka zaidi.



Waziri Mchengerwa akizungumza  baada ya kuunda kamati hiyo kwa mamlaka aliyopewa kwa mujibu wa kifungu cha 38 (1) na (2) ya Sheria ya Uhifadhi wa Wanyamapori sura ya 283 pia amesisitiza Uadilifu na weledi katika Utendaji kazi 


Waziri Mchengerwa ameitaka Kamati hiyo kuondoa changamoto zote ili tasnia ijiendeshe kibiashara na kupunguza urasimu na mikinzano isiyokuwa na tija kwa Taifa.


“Ni imani yangu kwamba, kwa kuzingatia ushauri utakaotolewa na Kamati hii tasnia ya Uwindaji wa Kitalii itazidi kuimarika na kuvutia wawekezaji wa ndani na nje ya Nchi"alisema


Mchengerwa ambaye pia tangu kuongoza Wizara kumekuwepo na maboresho makubwa ya Utendaji na kuongeza mapato alisema kamati inapaswa kuhakikisha vitalu vyote vinapata wawekezaji ili kuongezea mapato ya Serikali ikiwa ni pamoja na vitalu 43 ambavyo kwa sasa vipo wazi.



Alisema anatarajia Kamati hiyo itafanya kazi kwa ufanisi na weledi katika utendaji kwa kuzingatia kuwa imesheheni wataalamu kutoka katika nyanja mbalimbali.


Amefafanua kuwa uwindaji wa kitalii unachangia katika pato la Taifa hususani fedha za kigeni na kwamba kwa wastani, Serikali inakusanya takriban shilingi Bilioni 30 kwa mwaka kutokana na Uwindaji wa huo na unachangia ajira za rasmi na zisizo rasmi kwa jamii.


Alisema kiasi hicho ni kidogo ukilinganisha na utajiri wa raslimali za wanyamapori hapa nchini ambapo ameitaka Kamati hiyo  kufanya kazi na kujiwekea malengo  makubwa zaidi.


Ameitaka Kamati hiyo kuzitambua  changamoto zinazokabili tasnia hiyo ili kuja na mikakati ambayo itasaidia kuboresha  sekta  hiyo.


Amezitaja baadhi ya changamoto hizo kuwa ni pamoja na  mabadiliko ya Sera na Sheria za  Mataifa yanayoleta watalii wengi wa uwindaji, mabadiliko ya tabia nchi,uvamizi wa mifugo katika vitalu vya uwindaji wa kitalii hivyo kuathiri ustawi wa tasnia hii, na kampeni za wapingaji wa uwindaji wa kitalii ambazo kwa kiasi kikubwa zimeingilia maamuzi ya Mkataba wa Kimataifa unaosimamia Biashara ya Wanyamapori na Mimea iliyopo Hatarini kutoweka (CITES).


Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Ushauri wa Ugawaji Vitalu

Profesa Jafary Kideghesho, amemhakikishia  Waziri Mchengerwa  kuwa Kamati yake itafanya kazi kwa weledi ili kufikia  maono na Serikali ya kutaka tasnia  hiyo  kuchangia  katia uchumi.


Naye Katibu wa Kamati hiyo ambaye pia ni Kamishna wa Mamlaka ya Wanyamapori nchini (TAWA) Mabula Nyanda amemshukuru Mhe. Mchengerwa  kwa kuiunda Kamati  hiyo ambapo amesema  itasaidia kuboresha  tasnia hiyo kwa kuwa imejumuisha  wataalaam waliobobea  katika tasnia hiyo.


Mara baada ya uzinduzi huo waziri Mchengerwa ametoa  nyaraka  na miongozo mbalimbali kwa wajumbe wote ikiwa ni  namna ya kuwakabidhi nyenzo kwa ajili ya utekelezaji wa  kazi zao.


Uwindaji wa Kitalii ni miongoni wa Idara ambazo zimekuwa nyeti kwa Wizara hiyo na watendaji kadhaa wamekuwa wakiingia katika migogoro kutokana na maamuzi Yao katika sekta hiyo.


Ili kupunguza migogoro Wizara hiyo ilianzishwa mfumo wa kugawa vitalu kutokana na mnada wa kielekroniki ambao hata hivyo bado unachangamoto .





No comments: