Matukio ya ukiukwaji haki za binaadamu mwaka 2025 yametia doa Taifa. - MAIPAC MEDIA TANZANIA

Breaking

MAIPAC MEDIA TANZANIA

A Centre for Indigenous and Pastoralists Community Informations




Monday, 20 April 2026

Matukio ya ukiukwaji haki za binaadamu mwaka 2025 yametia doa Taifa.

 

Mkurugenzi wa LHRC,  Wakili  Dk Anna Henga

Mratibu wa Utafiti wa LHRC, Wakili Fundikira Wazambi  


Mwandishi wetu, Arusha


maipacarusha20@gmail.com 


Matukio ya Ukiukwaji wa Haki za Binaadamu  Nchini, ikiwepo mauwaji, utekaji, uhuru wa vyombo vya habari, uhuru wa kukusanyika , kujichukulia sheria mkononi kwa wananchi  yameongezeka kwa kiasi kikubwa na "kutia doa" Taifa la Tanzania.


Hayo yamebainishwa katika  ripoti  ya hali za haki za binaadamu  2025, ambayo imetolewa leo April 20, 2026  na Kituo cha Sheria na Haki za binadamu (LHRC) na Shirika la Zanzibar Fighting Against Youth Challenge Organization (ZAFAYCO), 


Akisoma ripoti hiyo, Mratibu wa Utafiti wa LHRC, Wakili Fundikira Wazambi  amesema, miongoni mwa matukio makubwa ya ukiukwaji wa haki za binaadamu, yaliyotokea mwaka jana ni vurugu za uchaguzi mkuu, ambapo mamia ya watu waliuawa, wengine kujeruhiwa, wengine kukamatwa na mali nyingi kuharibiwa.


Wakili Wazambi pia alisema kwa mwaka jana pia kimekuwepo na ongezeko la matukio ya utekaji ambapo watu 197    kwa kipindi cha miaka mitano waliliripotiwa kutekwa  huku idadi kubwa ikiwa ni mwaka jana.


Amesema pia mwaka jana, kumekuwepo na  matukio ya kuminya uhuru wa vyombo vya habari,  kufungwa inteneti, kufungwa mitandao ya kijamii, kuingiliwa uhuru wa kuabudu ikiwepo kufungwa makanisa ya ufufuo na uzima na kuingiliwa uhuru wa vyama vya siasa wakati wa uchaguzi na baada ya uchaguzi.


Akizungumza  wakati wa uzinduzi wa ripoti hiyo, Mkurugenzi wa LHRC,  Wakili  Dk Anna Henga amesema  Machafuko yaliyotokea wakati na baada ya uchaguzi Mkuu Oktoba 2025, siku ya uchaguzi na baada ya uchaguzi yaliibua hisia na wasiwasi mkubwa kuhusu ulinzi wa haki za msingi za binadamu, ikiwemo haki ya kuishi na haki ya kukusanyika kwa amani.


Amesema ripoti ya hali ya haki za binaadamu mwaka jana, inaonesha ongezeko la matukio ya utekaji na upoteaji wa watu, ambapo LHRC ilikusanya matukio 80 mwaka 2025, yakihusisha wanasiasa na wananchi wa kawaida.


Wakili Dk Henga pia amesema kulikuwepo na ukiukwaji wa haki za kidigitali ikiwemo uminyaji na uzimaji wa internet na upatikanaji wa majukwaa ya mtandaoni wakati wa kipindi cha uchaguzi, hali iliyodhoofisha uhuru wa kujieleza na upatikanaji wa taarifa.


Taarifa kamili ya ripoti ya hali ya haki za binaadamu mwaka 2025 itapatikana hapa.

https://humanrights.or.tz/en/post/resources-center/thrr2025


No comments: