Mwandishi Wetu maipac
maipacarusha20@gmail.com
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) leo Agosti 13, 2026, imelielekeza Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii kuendeleza mikakati ya kuboresha uwekezaji katika maeneo ya Hifadhi za Taifa nchini, Kuboresha miundombinu, na kuongeza mazao mapya ya utalii ili kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea Tanzania pamoja na mapato yatokanayo na shughuli za utalii.
Maelekezo hayo yametolewa na Kaimu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Rashid A. Shangazi (Mb) katika kikao kilichofanyika Bungeni Dodoma kikiwa na lengo la kupitia na kujadili masuala mbalimbali yanayohusu utekelezaji wa miradi ya uwekezaji katika Hifadhi za Taifa, uhifadhi, utalii pamoja na mikakati ya kuongeza mchango wa sekta ya utalii katika kukuza uchumi wa Taifa.
![]() |
Kikao hicho kilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Wizara wakiongozwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii Bw. Nkoba E. Mabula, viongozi kutoka Ofisi ya Msajili wa Hazina pamoja na Menejimenti ya TANAPA ikiongozwa na Kamishna wa Uhifadhi, Massana G. Mwishawa.
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) ni miongoni mwa Kamati za Kudumu za Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yenye jukumu la kusimamia na kushauri kuhusu mwenendo wa uwekezaji wa mitaji ya umma kwenye mashirika, kampuni na taasisi za umma zilizoko chini ya uratibu wa Ofisi ya Msajili wa Hazina.



No comments:
Post a Comment