RC MAKALLA AAGIIZA KAMATI ZA MAAFA ARUSHA KUJIANDAA NA MVUA ZA ELNINO - MAIPAC MEDIA TANZANIA

Breaking

MAIPAC MEDIA TANZANIA

A Centre for Indigenous and Pastoralists Community Informations




Wednesday, 26 August 2026

RC MAKALLA AAGIIZA KAMATI ZA MAAFA ARUSHA KUJIANDAA NA MVUA ZA ELNINO

 

Mkuu wa Mkoa wa Arusha CPA Amoss Makalla Amezitaka Mamlaka ya Hifadhi  Ngorongoro na TANAPA kushirikiana na TANROAD kuhakikisha  barabara kwenye maeneo ya Hifadhi zinapitika



RC Makkala Amezitaka TANROAD, TARURA,  kushughulikia na kuboresha miundombinu ya barabara, madaraja, vivuko, makaravati na  kuzibua mitaro


 


Mwandishi Wetu 


maipacarusha20@gmail.com 


Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe.CPA Amos Gabriel Makalla amewaagiza wakuu wa wilaya za Mkoa wa Arusha na Kamati zao za Usalama kujipanga kukabiliana na uwepo wa mvua za Elnino zinazotarajiwa kunyesha kuanzia mwezi Septemba 2026 kulingana na taarifa za Mamlaka ya Utabiri wa hali ya hewa nchini.


Mhe. Makalla ametoa maelekezo hayo kufuatia agizo la Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa wakuu wa Mikoa kujiandaa kukabiliana na Maafa yatakayotokana mvua za Elnino, kwenye kikao cha Kamati za Usalama Mkoa na wilaya za Ngorongoro na Karatu kilichofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano Ofisi za Makao Makuu ya Mamlaka ya Uhifadhi Ngorongoro leo Agosti 26,2026 


CPA Makalla amewataka wakuu wa wilaya wote kukaa vikao na Kamati za Maafa za wilaya na kuandaa mkakati wa kukabiliana na mvua hizo na kuzitaka Taasisi za binafsi, za Serikali na wadau wote kuandaa mkakati wa kukabiliana na madhara yatakayotokana na mvua hizo za Elnino


"Angalieni viashiria hatarishi kwenye Taasisi kama shule na vyuo, Mamlaka ya Uhifadhi Ngorongoro na TANAPA zenye dhamana ya Utalii, hakikisheni usalama wa barabara kwenye maeneo ya Hifadhi ili kuepuka kukwamisha shughuli za utalii, TANROAD na TARURA anzeni ukarabati kwenye maeneo korofi na hatarishi hususani kwenye madaraja ambako ni mapitio ya maji mengi ili kuzuia maafa wakati wa mvua hizo." Amesema CPA Makalla.


Awali CPA Makalla amezitaka Kamati za Usalama wilaya kuimarisha usalama kwenye  maeneo yote kufuatia Mikutano ya Kimataifa inayotarajiwa kufanyika mkoani Arusha mwezi Septemba mpaka Novemba 2026 ikiwemo Mkutano wa Mabunge ya Dunia (IPU) Mkutano wa Uzinduzi wa  Afya ya Msingi nchi za Afrika pamoja na  Mkutano wa  Dunia wa Hotikacha.

No comments: