TUME YA HAKI ZA BINADAMU NCHINI YAWASIKILIZA WAANDISHI WA HABARI WALIOKAMATWA KWA KUANDIKA HABARI ZA NGORONGORO - MAIPAC MEDIA TANZANIA

Breaking

MAIPAC MEDIA TANZANIA

A Centre for Indigenous and Pastoralists Community Informations




Thursday 23 March 2023

TUME YA HAKI ZA BINADAMU NCHINI YAWASIKILIZA WAANDISHI WA HABARI WALIOKAMATWA KWA KUANDIKA HABARI ZA NGORONGORO

 

Baadhi ya waandishi wa Habari wakiwa katika picha ya pamoja na Tume ya Haki za Binadamu nchini mara baada ya kusikiliza hali ya ukiukwaji wa haki za binadamu

 

Mussa Juma Mwandishi wa Gazeti la Mwananchi Mkoani Arusha akieleza hali ya ukiukwaji wa haki za Binadamu Kwa waandishi wa habari Ngorongoro

Mkurugenzi wa Pingos Forum Edward Porokwa akieleza ukiukwaji wa haki za binadamu kwa tume ya haki za binadamu nchini ilipokutana na kundimla waandishi wa Habari Mkoani Arusha



Profit Mmanga mwandishi wa Habari wa Wasafi Media Mkoani Arusha akieleza tume ya haki za Binadamu nchini namna alivyokamatwa mara baada ya kuandika habari za wananchi wa Ngorongoro na kuhakiwa na Runinga yake ya Mtandaoni




NA: Andrea Ngobole, Arusha

maipacarusha20@gmail.com

Katika utekelezaji wa kufuatilia ukiukwaji wa haki za binadamu nchini Tanzania leo Tume ya haki za binaadamu na Utawala bora  nchini (THBUB), imekutana na waandishi wa habari mkoani Arusha, waliowahi kuathirika baada ya kuandika habari za mgogoro wa ardhi wa Loliondo na Ngorongoro.


 Tume hiyo iliyopo katika ziara ya kutembelea wilaya ya Ngorongoro kufahamu uwekaji wa mipaka Loliondo na kuhamishwa kwa wakazi wa Ngorongoro kwenda Msomera kama kuna ukiukwaji wa haki za binadamu,  imeamua kukutana na wanahabari waliowahi kufanyiwa vitendo vya ukiukwaji wa haki za binaadamu, baada ya kupokea wito kutoka wa asasi za kutetea haki za binaadamu mkoani Arusha.
 
Jaji mstaafu Mathew  Mwaimu (upande wa kushoto) ambaye ni mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu nchini akisikilza maelezo ya baadhi ya waandishi waliokumbwa na madhila ya ukiukwaji wa haki za Binaadamu baada ya kuandika habari za Ngorongoro na Loliondo


Mwenyekiti wa tume hiyo, Jaji mstaafu Mathew Mwaimu, alisema walikuwa Loliondo na Ngorongoro kuwasikiliza wananchi na wakapata maombi kuja kuwasikiliza na wanahabari ambao kwa namna moja ama nyingine wameathirika na matukio ya Loliondo na Ngorongoro.

 
Lilian Oddo akiielezea Tume ya Haki za Binadamu alivyokamatwa na Polisi baada ya kuandika habari zinazohusu masuala ya Loliondo 
 
Wakizungumza na tume hiyo, wanahabari  Julius Msagati(star Tv), Lilian Oddo( Leo Tv) na Profit Mmanga( Wasafi TV) walieleza tume hiyo waliwahi kukamatwa na kuwekwa rumande kutokana na kuandika habari za Ngorongoro.

Msagati alisema mnamo mwezi june mwaka jana, akiwa na waandishi wengine, walialikwa na wananchi katika kijiji cha Nainokanoka ndani ya eneo la Mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro na baada ya mkutano na wananchi walikamatwa na askari wa mamlaka hiyo.

"Tulikamatwa tukapekuliwa kwa zaidi ya masaa matano bila kuelezwa makosa yetu na baada ya mlalamiko kufika ngazi mbali mbali tuliachiwa saa nne usiku kutoka Ngorongoro"alisema

Mwanahabari Oddo na Mmanga walieleza kukaa rumande kituo kikuu cha polisi Arusha, kitengo cha Utalii kwa siku mbili baada ya kukamatwa kutokana na kuandika habari za wananchi kuhusiana na zoezi la kuhamishwa wananchi wa tarafa ya Ngorongoro kwenda Msomera.

"tulikamatwa maeneo tofauti kama wahalifu na kupelekwa polisi na tuliandika maelezo, lakini baada ya siku mbili tulitolewa na Waziri wa mambo ya ndani, Hamad Masauni ambaye alikuwa kwenye ziara Arusha hasa baada ya malalamiko ya wanahabari"alisema

Alisema licha ya kuachiwa Runinga yake ya mtandao aliyokuwa anaisimamia ya Leo Tv iliondolewa mtandaoni.
 
Mwandishi wa habari mwandamizi wa Star TV mkoani Arusha, Angelo Mwolekwa akieleza hali ya ukiukwaji wa haki za binadamu katika kukuasanya taarifa za wakazi wa Ngorongoro na Loliondo


Mwandishi mwandamizi wa star tv, Angelo Mwoleka alisema wakati wa zoezi la kuwahamisha wananchi wa Ngorongoro na kumegwa eneo la loliondo kuanzishwa pori la akiba Pololeti kumekuwepo na ukiukwaji wa haki za binaadamu.

Mwoleka alisema wanahabari walikuwa wakipokea simu ya vitisho kutoandika habari za wananchi na badala yake waandishi maalum walipewa jukumu la kuandika habari za upande mmoja tu na hivyo kuwanyima haki watanzania wengi kujua ukweli.

Mkurugenzi wa shirika la Uraia na msaada wa kisheria(CILAO) Odero Charles aliomba tume hiyo, kutenda haki katika sakala hilo kwani kuna matukio mengi ya ukikwaji haki za binaadamu ikiwepo wananchi kuporwa ardhi na mmoja kupotea.

"Tunaimani kubwa na tume hii kutoa taarifa ya haki ambayo itakwenda kuondoa tatizo la migogoro ya ardhi hasa pale ambapo serikali inakiuka sheria na kuchukuwa ardhi ya wananchi bila maridhiano kwa madai ya kufanya uhifadhi ama kuwapa wawekezaji"alisema.

Tume ya Haki za binaadamu na Utawala bora imefika Arusha na kutembelea Loliondo na Ngorongoro, ikiwa ni takriban miezi mitatu tangu tume ya afrika ya haki za binaadamu nayo kutembelea maeneo hayo kuzungumza na wananchi kuhusiana na tuhuma za ukiukwaji wa haki za binaadamu.

 

No comments:

Post a Comment